• Idhaa ya Kiswahili
  • Uchumi
  • Michezo
  • Facebook
  • ChinaABC
  • Sayansi
  • Afya
  • Makampuni kutoka China yaahidi fursa zaidi Afrika kupitia mfumo wa Mkanda Mmoja Njia Moja

    (GMT+08:00) 2017-06-06 16:39:48
    Na Eric Biegon katika Chengdu, Sichuan

    Wiki tatu tu baada ya kumalizika kwa kongamano la kwanza kabisa kuhusu Mkanda Mmoja Njia Moja mjini Beijing, makampuni makubwa ya Kichina yameelezea utayari wao wa kuongeza uwekezaji katika nchi ambazo hadi sasa yamejiunga katika mpango huo.

    Makampuni hayo, ambayo yanamilikiwa na serikali ya China, yana Imani kuwa mufumo huu mpya wa ushirikiano utatoa fursa zaidi za kiuchumi, kijamii na kisiasa kati ya nchi husika na China, ambayo ni uchumi wa pili kwa ukubwa duniani.

    Afrika kwa sasa inashuhudia kuongezeka kwa kasi kwa miundombinu na maendeleo ya viwanda. Miradi mashuhuri katika eneo hili yanatekelezwa na makampuni ya Kichina.

    Katika kilele cha kongamano hilo la Mkanda Mmoja Njia Moja, Viongozi wa dunia waliojumuika pamoja waliazimia kuweka mkazo mkubwa kwa tatizo la miundombinu mbovu na ukosefu wa fedha kwa ajili ya miradi muhimu, hasa katika bara la Afrika.

    Wiki iliyopita, labda kuhakikisha harakati hizo zimengoa nanga, baadhi ya makampuni ya Kichina yenye makao makuu yao katika mji wa Chengdu, Mkoani Sichuan, zilitangaza mipango ya kupanua shughuli zao katika Afrika.

    Mojawapo ya makumpuni hizo, China Railway Engineering Group Company Limited, imefichua kuwa itapanua shughuli zake katika Afrika marudufu katika miaka kumi ijayo. Kampuni hiyo ni maarufu kwa ujenzi wa reli za kisasa.

    "Kampuni ya China Railway No. 2 ni mwanakandarasi muhimu wa ujenzi katika Afrika, na kampuni yetu inatarajia fursa zaidi ya kushiriki katika ujenzi wa Afrika." Akasema bwana Liao Zhiming, ambaye ni Mkurugenzi Mkuu wa China Railway No.2 Engineering Group. Hii, kwa mujibu wa mkurugenzi huo mtendaji itainua jukumu la kukuza urafiki, mawasiliano, na ushirikiano kati ya China na Afrika.

    CREGC, kama inavyofahamika China, hata hivyo haishiriki tu katika ujenzi wa reli. Shughuli zake zingine ni pamoja na uhandisi, ujenzi wa miundombinu na usimamizi, maendeleo ya mali isiyohamishika, miradi ya kimataifa na biashara, utafiti, na kubuni na ushauri, biashara pamoja na biashara ya ujenzi wa vifaa vya maendeleo. Kampuni hii inasema ina nia ya kuanzisha baadhi ya, kama sio, miradi yote katika sekta hizi, barani Afrika.

    Kampuni nyingine kutoka Sichuan ambalo limeangaza jicho lake Afrika ni lile la Dongfang Electronic Corporation. Maarufu kama DEC, kampuni hii ni maarufu duniani kwa kutengeneza vifaa vya kuzalisha nguvu za umeme pamoja na kutoa kandarasi kuhusu ujenzi wa chemichemi za nishati. Kampuni hii ya umeme inahusika katika jitihada za kuzalisha nishati safi. Inafahamika kwa uwezo wake mkubwa hasa katika kuzalisha umeme wa maji, mafuta, nyuklia, gesi, upepo na vifaa vya nishati ya jua.

    Wakurugenzi wa kampuni hiyo wanasema wanaelewa vikwazo vya nishati barani Afrika. Kwa maoni yao, Dongfang Electric Corporation ina uwezo wa kushughulikia upungufu wa umeme kila kote Afrika. Kampuni hiyo, sawia na waangalizi wengi, ina maoni kwamba itakuwa jambo lisilowezekana sana kwa Afrika kufanikiwa katika sekta ya viwanda kama ilivyoainishwa katika mfumo wa Mkanda Mmoja Njia Moja chini ya hali ya sasa ya uwezo wa kuzalisha umeme.

    Nafasi za Ajira

    Makampuni zote mbili, hata hivyo, zimekiri kwamba miradi hizi zinaweza tu kufanikiwa iwapo jamii zitashirikishwa pakubwa katika nchi ambazo miradi mbalimbali zitatekelezwa.

    Kwa muda sasa, makampuni ya Kichina zilizoko na oparesheni Afrika zimekuwa zikituhumiwa kwa kusafirisha wafanyikazi wake kutoka China na kutohusisha jamii zilizoko katika maeneo ya miradi yao. Afisa mtendaji wa China Engineering, hata hivyo, ana maoni tofauti.

    Bwana Liao Zhiming kutoka CREGC ama kwa kweli, anasisitiza kwamba mafunzo na fursa za ajira mbalimbali yamekuwa yakitolewa na makampuni zinazotoka China. Kwanza, alitaka kufafanua kuwa miradi mikubwa zinazotekelezwa na makampuni ya Kichina zinahitaji ujuzi fulani ambayo kwa mara nyingi wengi kutoka mataifa ya Afrika hawana.

    "Katika hatua za mwanzo, sisi tunatumia wafanyakazi wa Kichina kwa sababu ya muda mdogo wa kukamilisha miradi. Hii haina maana kwamba sisi hatuthamini kazi ya wakazi wa mataifa hayo." Alisema Zhiming.

    Zhiming anasema makampuni ya Kichina yanalazimika kutoa mafunzo kwa wakazi kuhusu mahitaji ya mradi. Yeye anasema kuwa wafanyakazi wote lazima waelewe ubunifu unaohitajika. Na hili kuafikia hayo, ni lazima kwanza watoe mafunzo yao.

    Mkuu huyo wa China Engineering Group alitoa mfano wa miradi zilizoko Addis Ababa, Ethiopia ambazo zilitekelezwa na CREGC. Anasema miradi hii kwa kiasi kikubwa zimefanywa na wananchi walioajiriwa kwa idadi nzuri.

    "Nchini Ethiopia, sisi tulitia saini mkataba wa miaka mitatu kukamilisha moja ya miradi. Lakini ili kuongeza kujenga uwezo katika mwaka wa kwanza, tuliamua kutumia idadi sawa ya wenyeji ikilinganishwa na nguvu kazi ya Kichina wenye ujuzi wetu katika mfumo wa "one plus one" (1 + 1). Hii inasaidia sana katika kukuza ufanisi." Alieleza.

    Utaratibu huu kulingana na Zhiming inasaidia wenyeji kupata ufahamu wa miradi. Katika mwaka wa pili, afisa huyo alisema nusu ya nguvu kazi ya Kichina ilihifadhiwa katika mradi, wakati nusu nyingine ilirudishwa nyumbani.

    Kufikia mwaka wa tatu, wataalamu ishirini tu wa Kichina walibaki Ethiopia kusaidia kukamilisha mradi. Mafundi hao 20, kwa mujibu wa Zhiming, walikuwa tu wanabakia kusaidia mafundi wa ndani wao wakiendelea kujenga mradi huo.

    Katika mradi huu moja, Zhiming anasema wenyeji 600 walipata mafunzo na kuajiriwa na kampuni yake. Anasisitiza kwamba hii ni mfano wa kuigwa ambayo imekuwa ikitekelezwa na makampuni ya Kichina ambayo zilianzisha shughuli katika nchi zinazoendelea.

    "Serikali yetu inahimiza makampuni ya Kichina kutumia wenyeji wengi iwezekanavyo ili kukuza ajira za ndani." Anasema.

    Afisa huyo hata hivyo alibainisha kwamba wana wajibu wa kutekeleza miradi yenye ubora wa hali ya juu. Anasema miradi yote zinazofanywa na makampuni ya Kichina hayana dosari, akielezea kuwa wanatilia mkazo mkubwa kwa ubora wa mradi.

    "Sisi tunafuata kanuni ya ubora wa miradi katika China. Tunafanya hivyo kwa mataifa ambayo tumeanzisha shughuli zetu. Mimi ninafurahi kusema kwamba miradi zilizofanywa na makampuni ya Kichina ni ya daraja ya juu ya kufuzu." Alisema.

    Wasimamizi wa makampuni hizi mbili ya serikali ya China wanashikilia kuwa mpango wa Mkanda Mmoja Njia Moja itawapa uwezo watu kupitia fursa mbalimbali ikilinganishwa na mifano ya awali ya ushirikiano iliyotumiwa na China na washirika wake.

    Chini ya mfumo huu wa kiuchumi wa Mkanda Mmoja Njia Moja, China imekaa katikati huku taasisi za Kichina zinazoshughulika katika nyanja mbalimbali kama vile biashara, matibabu, elimu, utamaduni, miundombinu, nishati, kilimo, viwanda, fedha kati ya mengine, yakipewa jukumu na wajibu wa kuharakisha na kuhakikisha utekelezaji wa miradi yenye mafanikio miongoni mwa nchi zinazohusika.

    Webradio
    Sauti
    6:00-7:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 1
    12:00-13:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 2
    20:00-22:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 3A
    • FM 3B
    Maoni yako