• Idhaa ya Kiswahili
  • Uchumi
  • Michezo
  • Facebook
  • ChinaABC
  • Sayansi
  • Afya
  • Wachina washauriwa kuwekeza zaidi Tanzania kufaidika na fursa EAC, SADC

    (GMT+08:00) 2019-09-06 10:25:31

    Na Majaliwa Christopher, Dar es Salaam

    TANZANIA kupitia Mamlaka ya Ukanda Maalumu wa Uwekezaji (EPZA) imewakaribisha wawekezaji kutoka China kuwekeza nchini humo wakati huu ambapo Serikali inalenga kufanya nchi hiyo ya Afrika ya Mashariki kuwa kitovu cha viwanda kutokana na faida iliyo nayo ya kijiografia.

    Mkurugenzi Mkuu wa EPZA Joseph Simbakalia akizungumza na wafanyabiashara kutoka jimbo la Shandong, China waliotembea jijini Dar es Salaam Alhamisi, Septemba 5, 2019, aliueleza ujumbe huo wa wafanyabiashara kuwa kuwekeza nchini Tanzania kuna faida kubwa ya upatikanaji wa soko la uhakika pamoja na malighafi.

    Bw. Simbakalia alisema Tanzania ni mjumbe wa Jumuia ya Afrika Mashariki (EAC) Pamoja na Jumuia ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) hivyo kuwekeza katika nchi hiyo ya Afrika ya Mashariki kunampa mwekezaji fursa kubwa ya kupata soko la uhakika.

    Bw. Simbakalia aliongeza kuwa EPZA imejipanga kuhakikisha kuwa viwanda ambavyo vipo tayari vinaongeza uzalishaji ili kuweza kusafirisha na kuuza katika maeneo yote ya jumuia za EAC na SADC.

    "Hadi sasa Viwanda vyote vilivyoko chini ya Ukanda Maalum wa Uwekezaji vinauza bidhaa katika Masoko ya nje ya Tanzania," alisema.

    Aliongeza kuwa kuwekeza nchini Tanzania kunamaanisha kuwa mwekezaji anapata fursa ya ya moja kwa moja kuuza bidhaa zake katika nchi za Afrika ya Mashariki na Kusini ukizingatia kuwa nchi hizo ni rahisi kufikika kwa njia ya reli ya kati na ya TAZARA.

    Alieleza kuwa kampuni ya Tooku Garment Production ya China ambayo imewekeza katika EPZA inayozalisha suruali za jeans hadi sasa uzalishaji wake umefikia 600,000 kwa siku.

    Hata hivyo Bw. Simbakalia alisema kuwa mwakani, 2020 wanategemea kuongeza uzalishaji hadi kufikia 1,000,000 na kuongeza nafasi za ajira hadi kufikia zaidi ya 5,000 kutoka 2,700.

    Naibu Mkurugenzi wa Idara ya Biashara Jimbo la Shandong Bw. Lyu Wei aliishukuru EPZA kwa taarifa inayoelezea umuhimu wa kuwekeza katika eneo la EPZA na kuahidi kuwa watatoa maamuzi ya baadaye baada ya kumaliza ziara yao nchini Tanzania.

    Ziara hiyo ya wafanyabiashara kutoka China uliandaliwa na Idara ya Biashara ya Shandong kushirikiana na Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) and kampuni ya East Africa's Commercial and Logistics Centre Chamber of Commerce (EACLCCC).

    Meneja wa Kampuni ya EACLCCC Bi Cathy Wang alisema ziara hiyo inayohusisha wafanyabishara na ujumbe kutoka serikalini wapatao 80 unalenga kuangalia fursa za uwekezaji Tanzania bara na Zanzibar.

    Webradio
    Sauti
    6:00-7:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 1
    12:00-13:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 2
    20:00-22:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 3A
    • FM 3B
    Maoni yako