• Idhaa ya Kiswahili
  • Uchumi
  • Michezo
  • Facebook
  • ChinaABC
  • Sayansi
  • Afya
  • China kutoa $ 42.6M ujenzi makao makuu ya ulinzi Tanzania

    (GMT+08:00) 2019-11-26 09:43:47

    Na Majaliwa Christopher

    SERIKALI ya Jamhuri ya Watu wa China imetenga jumla ya Dola za Kimarekani Milioni 42.6 (Yuan Milioni 300) kwa ajili ya ujenzi wa makao makuu ya ulinzi jijini Dodoma, Tanzania.

    Hayo yamebainishwa Jumatatu, Novemba 25, 2019, jijini Dodoma na Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi (CDF) wa Tanzania, Jenerali Venance Mabeyo katika halfa ya uzinduzi wa ujenzi wa makao makuu ya ulinzi.

    Jenerali Mabeyo alisema kuwa kutengwa kwa fedha hizo na Serikali ya China inakuja kufatia safari yake ya kikazi aliyofanya katika nchi hiyo ya Asia ya Mashariki mwaka jana, 2018.

    Alibainisha kuwa akiwa nchini China, kwa mwaliko wa Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi wa nchi hiyo, walizungumzia mambo mbalimbali ya ushirikiano kati ya nchi hizo mbili katika nyaja ya ulinzi na usalama.

    Jenerali Mabeyo alibainisha kuwa akiwa nchini China pamoja na mambo mengine walizungumzia mambo mengi ikiwemo kuboresha zana za ulinzi pamoja na kusaidia ujenzi wa makao makuu ya ulinzi yenye hadhi na ubora wa kimataifa.

    "Lakini pia, ukizingatia kuwa hivi karibuni Rais (John Magufuli) alipandisha maaskari wengi vyeo na hatukuwa na magari ya kutosha kwa ajili ya maafisa hao," aliseme CDF Mabeyo, na kuongeza kuwa walijadili namna ya kusaidia kutatua changamoto hiyo.

    Alisema kuwa hivi karibuni Tanzania ilipokea magari 40 kutoka kwa Jeshi la Ukombozi la Watu wa China (PLA) kwa Jeshi la Ulinzi wa Tanzania (JWTZ).

    Magari hayo yalipokelewa na Rais wa Tanzania Dkt. John Magufuli, aliyesisitiza kuwa makabidhiano ya magari hayo yalikuwa ni kielelezo kingine tena cha uhusiano wa karibu, kidugu na kirafiki uliopo kati ya mataifa hayo mawili.

    Alibainisha kuwa tayari China ilituma timu ya wataalamu kufanya upembuzi yakinifu katika eneo ambalo makao makuu hayo ya ulinzi yatajengwa.

    "Misaada hii yote tunayopata kutoka China ni ishara kuwa ushirikiano wetu katika ulinzi na usalama kati yetu unazidi kuimarika na unakuwa kwa faida kwetu sote," alisema CDF Mabeyo.

    Mwezi Aprili mwaka huu, Balozi wa China nchini Tanzania Bi. Wang Ke na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) Dkt. Hussein Mwinyi waliweka jiwe la msingi la kuanza kwa ujenzi wa Chuo cha Taifa cha Ulinzi Tanzania awamu ya pili.

    China llilitoa msaada wa Shilingi Bilioni 56 za Tanzania kwa ajili kufadhili ujenzi wa chuo hicho.

    Msaada huo ulitolewa kupitia Jeshi la Ukombozi la Wananchi wa China na ulilenga kusaidia kuongeza idadi ya wanafunzi wa kozi fupi na ndefu kwa mafunzo ya viwango vya kimataifa.

    Webradio
    Sauti
    6:00-7:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 1
    12:00-13:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 2
    20:00-22:00 (Afrika Mashariki)
    • FM 3A
    • FM 3B
    Maoni yako