1: Ardhi, Maliasili na Idadi ya Watu

Ardhi ya taifa

Eneo la ardhi

Jamhuri ya Watu wa China yaani China, iko kwenye sehemu ya mashariki ya Bara la Asia na kando ya magharibi ya Bahari ya Pasifiki. Eneo la nchi kavu la China ni karibu kilomita za mraba milioni 9.6, ambayo ni nchi yenye eneo kubwa zaidi kwenye Bara la Asia, na ni nchi kubwa ya tatu duniani ikizifuata Russia na Canada.

Toka kaskazini hadi kusini, ardhi ya China inaanzia kwenye chanzo cha Mto Heilongjiang, kaskazini ya Mto Mo (digri 53.30 ya latitudo ya kaskazini) mpaka Zengmu Ansha ya ncha ya kusini ya Visiwa vya Nasha (digrii 4 ya latitude ya kaskazini), umbali kati ya kusini na kaskazini ni kilomita 5500; toka mashariki hadi magharibi, ardhi ya China inaanzia sehemu ya makutano kati ya Mto Heilong na Mto Usuri (digrii 135.05 ya longitudo ya mashariki), mpaka Uwanda wa juu wa Pamier (digri ya 73.40 ya longitude), umbali kati ya mashariki na magharibi ni kilomita 5000.

Mpaka wa nchi kavu ya China una urefu wa kilomita 22,800, upande wa mashariki, China inapakana na Korea ya kaskazini, upande wa kaskazini inapakana na Mongolia, upande wa mashariki inapakana na Russia, upande wa kaskazini magharibi inapakana na Kazakstan, Kyrgyzstan na Tajikstan, upande wa magharibi na wa kusini magharibi inapakana na Afgahnistan, Pakistan, India, Nepal, na Buthan, upande wa kusini inapakana na Myanmar, Laos na Vietnam. Na upande wa mashariki na wa kusini mashariki China inakabiliana kwa bahari na Korea ya kusini, Japan, Philipines, Burnei, Malaysia na Indonesia.

Bendera ya Taifa, Nembo la Taifa, Wimbo la Taifa na Mji Mkuu

Bendera ya Taifa

Bendera ya Taifa: Bendera ya Taifa la Jamhuri ya Watu wa China ni Bendera nyekundu yenye nyota tano za manjano, kiasi cha ulinganifu kati ya urefu na kimo cha bedera hiyo ni 3:2. Bendera ya Taifa ina rangi nyekundu ambayo inamaanisha mapinduzi. Nyota 5 zenye pembe 5 kwenye bendera hiyo ni za rangi ya manjano, na kila ncha ya nyota 4 ndogo zenye pembe 5 inaielekea katikakati ya nyota kubwa, ambayo inaonesha mshikamano mkubwa wa wananchi chini ya uongozi wa Chama cha kikomunisti cha China.

Nembo ya Taifa ya Jamhuri ya Watu wa China

Nembo ya Taifa ya Jamhuri ya Watu wa China: Nembo ya Taifa ya Jamhuri ya Watu wa China inaonesha Bendera ya Taifa, Uwanja wa Tian An Men, gurudumu lenye meno na mashuke ya ngano na mpunga, ambayo inamaanisha mapambano ya mapinduzi ya demokrasia mpya yaliyofanyika tokea harakati za "tarehe 4 Mei" mwaka 1919 na wananchi wa China pamoja na kuzaliwa kwa China mpya yenye utawala wa kidemokrkasi wa uumma chini ya uongozi wa tabaka la wafayakazi na kwenye msingi wa shirikisho la wafanyakazi na wakulima.

Wimbo wa Taifa

Wimbo wa Taifa wa Jamhuri ya Watu wa China ni wimbo wa "Songa mbele watu mliojitolea", ambao ulitungwa mwaka 1935, mtungaji wa maneno ya wimbo huu ni mwandishi maarufu wa tamthiria Bwana Tian Han, muziki wa wimbo huu ulitungwa na Bwana Nie Er ambaye alikuwa mwanzilishi wa harakati za muziki mpya wa China. Wimbo huo ulikuwa wimbo wa kauli mbiu ya filamu ya "Vijana waliokumbwa na mashambulizi". Filamu hiyo ilieleza kuwa baada ya tukio la "Tarehe 18 Septemba" mwaka 1931, Japan iliposhambulia na kuikalia mikoa mitatu ya kaskazini mashariki ya China, taifa la China lilikuwa katika kipindi cha kufa na kupona, ambapo baadhi ya vijana walijitoa kutoka kwenye hali ya uchungu na mahangaiko wakaenda kwenye medani ya vita kupambana na mashambulizi ya Japan. Kutokana na filamu hiyo, wimbo huu uliimbwa na wachina wa kila sehemu nchini China, ukasifiwa kuwa mbiu wa kutoa mwito wa kujipatia ukombozi wa taifa la China.

Tarehe 27 Septemba mwaka 1949, mkutano wa kwanza wa wajumbe wote wa Baraza la mashauriano ya kisiasa la umma la China ulipitisha azimio kuwa kabla ya kutungwa rasmi kwa wimbo wa taifa wa Jamhuri ya Watu wa China, wimbo wa "Songa mbele watu mliojitolea" uwe wimbo wa taifa. Tarehe 14 Machi, mwaka 2004, Mkutano wa pili wa Halmashauri ya kudumu ya 10 ya Bunge la umma la China ulipitisha mswada wa marekebisho ya katiba ukaamua kuwa wimbo wa Taifa wa Jamhuri ya Watu wa China ni wimbo wa "Songa mbele watu mliojitolea ".

Wimbo wa Taifa

Nyanyukeni!

Enyi msiokubali kuwa watumwa!

Tujenge ukuta mkuu mpya kwa damu na miili yetu!

Taifa la China limekuwa hatarini kabisa,

Kila mmoja analazimika kupaaza sauti ya mwisho.

Nyanyukeni, nyanyukeni, nyanyukeni!

Sote tuwe na nia moja,

Tusonge mbele bila kujali risasi na mizinga!

Tusonge mbele bila kujali risasi na mizinga!

Mbele! mbele! mbele!

Mji Mkuu wa Jamhuri ya Watu wa China

Mji mkuu wa Jamhuri ya Watu wa China ni Beijing.

Tarehe mosi Oktoba mwaka 1949 mwenyekiti Mao Zedong kwenye roshani ya Tian An Men alitangaza dunia nzima kuwa serikali kuu ya Jamhuri ya Watu wa China imeasisiwa! Tokea hapo, Beijing ukiwa mji mkuu pamoja na China mpya umefungua ukurasa mpya wa historia.

Mamlaka ya Bahari na visiwa

Mwambao wa nchi kavu ya China unaanzia mlango wa Mto Yalu wa Mkoa wa Liaoning wa kaskazini hadi Mlango wa Mto Beilun wa Mkoa wa Guangxi wa kusini, urefu wake ni kilomita 1,800. Hali ya kijiografia ya pwani za bahari ni tambarare, ambapo kuna bandari na ghuba nyingi zenye hali bora, na nyingi ni bandari ambazo maji yake hayawezi kuganda kwa mwaka mzima. Kuna bahari kubwa 5 za karibu nchini China kama vile Bahari ya Bo, Bahari ya Huang, Bahari ya Mashariki, Bahari ya Kusini pamoja na Sehemu ya Bahari ya Pasifiki ya mashariki ya Taiwan. Miongoni mwa hizo, Bahari ya Bo ni bahari ya ndani ya China. Sehemu ya Bahari ya Pasifiki ya mashariki ya Taiwan inaanzia Visiwa vya Xiandao vya kaskazini vilivyoko kusini magharibi ya Visiwa vya Ryukyu vya Japan, mpaka kwenye Mlango wa Bahari ya Bashi wa kusini.

Eneo la bahari la China ni pamoja na maji ya ndani na mamlaka ya bahari ya China, eneo lake la jumla ni zaidi ya kilomita 380,000. Maji ya ndani ya China ni eneo la bahari la Jamhuri ya watu wa China toka mstari wa mamlaka ya bahari unaoelekea upande wa nchi kavu hadi mwambao wa bahari. Upana wa mamlaka ya bahari ya China ni nautical maili 12 kuanzia mstari wa bahari.

Kwenye eneo la bahari ya China kuna visiwa zaidi ya 5000, eneo lake la jumla ni kilomita za mraba 80,000, mwambao wa visiwa ni kilomita za mraba 14,000. Miongoni mwao Kisiwa cha Taiwan ni kikubwa zaidi kuliko vingine vyote, eneo lake ni kilomita za mraba 36,000; Kisiwa cha Hainan ni cha pili kwa ukubwa wake, eneo lake ni kilomita za mraba 34,000. Visiwa vya Diaoyu na Visiwa vya Chiwei vilivyoko kwenye bahari ya kaskazini mashariki ya Kisiwa cha Taiwan ni visiwa vilivyoko kwenye sehemu ya mashariki kabisa ya China. Visiwa vya Dongsha, Visiwa vya Xisha, Visiwa vya Zhongshan na Visiwa vya Nasha vilivyoko kusini kabisa ya China vinaitwa kuwa ni visiwa mbalimbali vya Bahari ya Kusini.

Hali ya Jiografia

Hali ya JiografiaChina ni nchi yenye milima mingi, eneo la sehemu za milimani linachukua theluthi mbili ya eneo la jumla la nchi nzima. Sehemu hizo za milimani ni pamoja na ardhi milimani, vilima na nyanda za juu. Katika eneo lote la China ardhi ya milima inachukua 33 %, nyanda za juu 26 %, mabonde 19 %, tambarare 12 % na vilima 10 %.

Katika mamilioni ya miaka kadhaa iliyopita, Uwanda wa Juu wa Qinghai-Tibet ulikuwa kama nundu kwenye ardhi duniani, maumbo ya ardhi ya China yakatokana na uwanda huo. Ukiiangalia ardhi ya China kutoka angani, hali ya kijiografia ya China ni kama ngazi inayoelekea mashariki kutoka magharibi, inatelemka hatua kwa hatua. Kutokana na kugongana kati ya ardhi ya India na ardhi ya Ulaya na Asia, Uwanda wa Juu wa Qinghai-Tibet ulijitokeza siku hadi siku, mwinuko wake kwenye usawa wa bahari ni zaidi ya mita 4000, hivyo uwanda huo unaitwa kuwa ni "Paa la dunia", na kuwa ngazi ya kwanza kwenye ardhi ya China. Kilele kikuu cha Jomolangma cha Mlima Himalaya kwenye Uwanda wa Juu wa Qinghai-Tibet kina urefu wa mita 8848.13, ambacho ni kilele cha juu cha kwanza duniani. Ngazi ya pili inaundwa na Uwanda wa Juu wa Mongolia ya ndani, Uwanda wa juu wa Huangtu, Uwanda wa Juu wa Yungui pamoja na Bonde la Talimu, Bonde la Zhungeer na Bonde la Sichuan, wastani wa mwinuko wake kutoka usawa wa bahari ni mita 1000-2000. Ukipita ukingo wa mashariki wa ngazi ya pili ni ngazi ya tatu inayoundwa na Milima Daxinganling, Milima Taihan, Mlima Wu na Mlima Xuefeng inayoelekea pwani ya mashariki ya bahari ya Pasifiki. Katika sehemu ya mwinuko unaotelemka chini ya mita 500 hadi 1000, kuna Tambarare ya Kaskazini ya mashariki, Tambarare ya Kaskazini, na Tambarare ya eneo la katikati na chini ya mtitiriko wa Mto Changjiang, na katika sehemu ya ukingoni mwa tambarare hizo kuna milima mifupi na vilima. Mashariki ya sehemu hiyo ni sehemu inayoelekea kwenye bahari ya China yaani ngazi ya nne, ambapo kimo cha maji ya sehemu kubwa ni chini ya mita 200.

Milima

Milima mingi mikubwa na mirefu imekuwa kama "mifupa" ya ardhi ya China, na kuundwa kuwa mifumo mingi tofauti ya milima. Milima mikubwa maarufu ya China ni: Milima Himalaya, Milima Kunlun, Milima Tiansha, Milima Tanggula, Milima Qinling, Milima Daxinganling, Milima Taihang, Milima Qilian, na Milima Hengduan.

Milima Himalaya: Milima hiyo wa umbo wa upinde unatambaa kwenye sehemu ya mipaka kati ya China na India na Nepal, urefu wake ni zaidi ya kilomita 2400, mwinuko wake kutoka usawa wa bahari ni mita 6000, ambayo ni milima mikubwa na mirefu zaidi kuliko mingine yote duniani. Mwinuko wa kilele chake kikuu Jomolangma kutoka usawa wa bahari ni mita 8848.13, kilele hicho ni cha juu zaidi kuliko vingine vyote duniani.

Milima Kunlun: Milima hiyo inaanzia Uwanda wa juu wa Pamil katika upande wa magharibi, na upande wake wa mashariki unafikia kaskazini magharibi ya Mkoa wa Sichuan, China, urefu wake ni zaidi ya kilomita 2500, wastani wa mwinuko kutoka usawa wa bahari ni mita 5000-7000, kilele chake cha juu zaidi cha Gonggeer kina mwinuko wa mita 7719 kutoka usawa wa bahari.

Milima Tianshan: Milima Tianshan inasimama kwenye sehemu ya katikati ya Mkoa unaojiendesha wa Xinjiang Uygur wa kaskazini magharibi ya China, wastani wa mwinuko wake kutoka usawa wa bahari ni mita 3000-5000, kilele chake cha juu zaidi Tomoer kina mwinuko wa mita 7455.3 kutoka usawa wa bahari.

Milima Tanggula: Milima hiyo iko kwenye sehemu ya katikati ya Uwanda wa Juu wa Qinghai-Tibet, wastani wa mwinuko kutoka usawa wa bahari ni mita 6000, kilele chake cha juu zaidi Geladandong kina mwinuko wa mita 6621 kutoka usawa wa bahari, ambapo ni chanzo cha Mto Changjiang ambao ni mto mrefu zaidi nchini China.

Milima Qinling: Upande wa magharibi wa milima hiyo inaanzia mashariki ya Mkoa wa Gansu, upande wake wa mashariki kufika sehemu ya magharibi ya Mkoa wa Henan, wastani wa mwinuko wake ni mita 2000-3000 kutoka usawa wa bahari, kilele chake kikuu Taibai kina mwinuko wa mita 3767 kutoka usawa wa bahari. Milima hiyo ni mstari muhimu wa kijiografia kati ya kusini na kaskazini nchini China.

Milima Daxinganling: Upande wake wa kaskazini unaanzia sehemu iliyo karibu na Mto Mo wa mkoa wa Heilongjiang, kaskazini mashariki ya China, upande wake wa kusini unafika eneo la juu la Mto Laoha, umbali kutoka kusini hadi kaskazini ni kilomita 1000, wastani wa mwinuko wa kutoka usawa wa bahari ni mita 1500, kilele chake kikuu Huanggangliang kina mwinuko wa mita 2029 kutoka usawa wa bahari.

Milima Taihang: Toka kaskazini hadi kusini milima hiyo inatambaa kwenye ukingo wa mashariki ya Uwanda wa Juu wa Huangtu, urefu wake ni zaidi ya kilomita 400, wastani wa mwinuko kutoka usawa wa bahari ni mita 1500-2000, kilele chake cha juu zaidi Xiaowutaishan kina mwinuko wa mita 2882 kutoka usawa wa bahari.

Milima Qilian: Milima hiyo inatambaa katika sehemu ya ukingoni mwa kaskazini mashariki ya Uwanda wa Juu wa Qinghai-Tibet, wastani wa mwinuko wa kutoka usawa wa bahari ni zaidi ya mita 4000, na kilele chake kikuu kina mwinuko wa mita 5547 kutoka usawa wa bahari.

Milima Hengduan: Milima hiyo iko kwenye sehemu ya kusini mashariki ya Uwanda wa Juu wa Qinghai-Tibet na katika sehemu ya makutano kati ya mipaka ya mikoa mitatu ya Tibet, Sichuan na Yunnan, wastani wa mwinuko kutoka usawa wa bahari ni mita 2000-6000, kilele chake kikuu Gongga kina mwinuko wa mita 7556.

Milima Taiwan: Milima hiyo inapita upande wa mashariki ya Kisiwa cha Taiwan , wastani wa mwinuko wake kutoka usawa wa bahari ni mita 3000-3500, kilele chake kikuu Yushan kina mwinuko wa mita 3952 kutoka usawa wa bahari.

Zaidi ya hayo, nchini China pia kuna milima mingine maarufu kama vile Mlima Huang, Mlima Tai, Mlima Hua, Mlima Song, Mlima Heng, Mlima Ermei, Mlima Lu, Mlima Wudang na Mlima Yandang.

Mito

Nchini China kuna mito mingi, miongoni mwao mito zaidi ya 1500 ambayo kila mto ni wenye eneo la kilomita za mraba 1000. Mito hiyo inagawanyika katika mito ambayo maji yake yanatiririka na kuingia baharini na mito isiyoingia baharini. Eneo la mito ambayo maji yake yanaingia baharini, linachukua 64 % ya eneo la jumla la nchi kavu ya China. Mto Changjiang, Mto Huanghe, Mto Heilongjiang, Mto Zhujiang, Mto Liaohe, Mto Haihe na Mto Huihe ni mito ambayo maji yake yanatiririka kuelekea mashariki na kuingia kwenye Bahari ya Pasifiki; Mto Yaluzhangbujiang wa Tibet unatiririka kuelekea mashariki na kutoka nje, tena kuelekea kusini na kuingia bahari ya Hindi, ambapo unapita Bonde kubwa la kwanza duniani la Yaluzhangbujiang lenye urefu wa kilomita 504.6, na kimo cha mita 6009; Mto Erqisi wa Xinjiang ni mto ambao maji yake yanatoka nje na kuingia kwenye Bahari ya Arctic. Mito ile ambayo maji yao yanaingia kwenye maziwa au kupotelea kwenye jangwa na sehemu ya maji yenye chumvi, eneo lake linachukua 36 % ya eneo la jumla la eneo la nchi kavu ya China.

Mto Changjiang ni mto mkubwa wa kwanza wa China, urefu wake wa jumla ni kilomita 6300, ambao ni mto wa tatu kwa ukubwa duniani, ukiifuata Mto Nile wa Afrika na Mto Amazon wa Amerika ya kusini. Eneo la juu ya Mto Changjiang linapita milima na mabonde makubwa, ambapo maliasili nyingi ya maji zinalimbikizwa kwenye sehemu hizo. Mto Changjiang pia ni mto wa kimaumbile wa shughuli za uchukuzi toka mashariki hadi magharibi nchini China. Hali ya hewa ya eneo la katikati na chini la Mto Changjiang ni ya joto na unyevunyevu, kuna mvua za kutosha, na ardhi yenye rutuba, ambapo ni sehemu iliyoendelea kiviwanda na kilimo nchini China.

Mto Huanghe ni mto mkubwa wa pili wa China, urefu wa jumla wa mto huo ni kilomita 5464. Kwenye eneo la huo kuna malisho na mbuga na maliasili nyingi za madini, katika historia yake eneo hilo lilikuwa moja ya machimbuko muhimu ya ustaarabu wa zama za kale za China.

Mto Heilongjiang ni mto mkubwa wa kaskazini ya China, urefu wake ni kilomita 4350, miongoni mwake maji ya eneo la mto huo la kilomita 3101 yanapita sehemu za nchini China.

Mto Zhujiang ni mto mkubwa wa kusini ya China, urefu wake ni kilomita 2214.

Mto Talimu wa kusini ya Xinjiang ni mto mrefu kabisa wa China ambao maji yake hayaingii baharini, urefu wake ni kilomita 2179.

Mbali na mito ya kiasili, nchini China pia kuna mfereji mmoja maarufu unaopita kusini na kaskazini. Mfereji huo ulichimbuliwa kwa nguvu za binadamu kuanzia karne ya 5, ambao ulianzia Beijing, kaskazini ya China hadi Hangzhou wa mkoa wa Zhejiang, mashariki ya China, mfereji huo unapitisha mifumo mitano mikubwa ya Mto Haihe, Mto Huanghe, Mto Huaihe, Mto Changjiang na Mto Qiantangjiang, urefu wa mfereji huo ni kilomita 1801, ambao ni mfereji mrefu zaidi kuliko mingine duniani uliochimbuliwa kwa nguvu za binadamu mapema zaidi duniani.


1 2 3 4 5