Wahamiaji 200 wafa pwani ya Libya
Wahamiaji zaidi ya 200 wanahofiwa kufariki baada ya boti lao kuzama kwenye bahari karibu na pwani ya Libya, shirika moja la Uhispania limesema.
Shirika hilo, Proactiva Open Arms, limesema maafisa wake walipata miili mitano ikielea karibu na boti mbili zilizokuwa zimezama, na ambazo zina uwezo wa kubeba zaidi ya watu 100 kila moja.
Afisa wa shirika hilo Laura Lanuza amesema miili ya watu hao watano waliyofanikiwa kuitoa baharini inaonesha walikuwa wanaume wa umri mdogo.
Msemaji wa kikosi cha majini cha Italia, ambacho huratibu shughuli za uokoaji, amethibitisha vifo vya watano hao.
Hata hivyo, amesema hawawezi kuthibitisha makadirio idadi ya waliofariki, kama yalivyotolewa na Proactiva kwa kuwa hawakupokea vilio vyovyote vya watu wakiomba msaada.
Shirika la kimataifa la uhamiaji (IOM) linasema zaidi ya wahamiaji 20,000 wamefika Italia mwaka huu kufikia sasa.
Watu 559 wanaaminika kufariki au kutoweka wakiwa safari kuelekea Ulaya kupitia eneo hilo.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |