Kampuni ya China kujenga makao makuu ya Umoja wa Posta Afrika
2019-12-31 09:24:42| CRI

Na Majaliwa Christopher

SERIKALI ya Tanzania imesaini mkataba na kampuni ya Beijing Construction Engineering Group kwa ajili ya ujenzi wa makao makuu ya Umoja wa Posta Afrika (PAPU).

Jengo la Umoja wa Posta Afrika litakalojengwa jijini Arusha, Kaskazini mwa Tanzania, litgharimu fedha za Kitanzania Shilingi Bilioni 33.5.

Utiaji saini mkataba wa mradi huo ulifanyika jijini Dar es Salaam Jumatatu, Disemba 23, 2019 ambapo ilielezwa kuwa fedha hizo kwa ajili ya ujenzi huo zinatolewa na Umoja huo pamoja na Serikali ya Tanzania.

Waziri wa Mawasiliano wa Tanzania Isack Kamwelwe akizungumza katika hafla hiyo alisema ujenzi wa jengo hilo ni fahari ya Tanzania na kwamba litalizidi kulitangaza taifa ndani na nje ya Bara la Afrika.

Alisema kwa kipindi kirefu tangu kuanzishwa kwa umoja huo mwaka 1980, kulikuwa na vute nikuvute kuhusu ujenzi wa jengo hilo hadi sasa, ambapo Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais Dkt. John Magufuli ilipoamua kulivalia njuga, na ujenzi huo unatarajiwa kukamilika ndani ya kipindi cha miaka mitatu.

Utiaji wa saini wa jengo hilo baina ya PAPU na mkandarasi kutoka Kampuni ya Beijing Construction Engineering Group (BCEG), pia ulishuhudiwa na Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), ambapo katika fedha za ujenzi huo, Tanzania imetoa asilimia 40 na asilimia 60 zimetoka PAPU.

Waziri Kamwelwe alisema wana imani kubwa na kampuni hiyo ya China kutokana na kuwa na uzoefu mkubwa katika kutekeleza miradi mbalimbali nchini Tanzania, hivyo wanaamini kuwa kazi hiyo itamalizika kwa muda uliopangwa na kwa ubora wa kimataifa.

Akiongea katika hafla hiyo, Mkurugenzi wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) Bw. James Kilaba alisema kuanza kuwa mradi huo umechukua muda mrefu kutoka na sababu mbalimbali.

"Kwa sasa tunaamini huu mradi utaanza mara moja na kukamilika ndani ya muda, hii ni alama muhimo kwa bara la Afrika na sekta nzima ya mawasiliano," alisema Bw. Kilaba.