SOKA: Cristiano Ronaldo kurejea tena kwenye ligi ya EPL
2021-05-24 18:18:53| cri

Cristiano Ronaldo anaripotiwa kutaka kukatiza hatma yake na Juventus na kuwa huru kurejea Man United. Mreno huyo anakumbana na hatma finyu na miamba hao wa Italia na amekuwa akihusishwa na kuondoka. Metro UK sasa inaripoti kuwa fowadi huyo anawazia kuungana tena na Mashetani Wekundu, chapisho hilo likiongezea kuwa mshindi huyo wa Ballon d'Or yuko tayari kupunguziwa mshahara wake kukamilisha hatua hiyo. Inaaminika kuwa United wanafuatilia hali yake ugani Turin ambapo akishindwa kufuzu kwa Ligi ya Mabingwa msimu ujao atalazimika kuondoka. Juve kwa sasa wanashikilia nafasi ya tano kwenye msimamo wa Serie A na alama 75 maana kuwa wanatakiwa kushinda mechi yao ya mwisho msimu huu dhidi ya Bologna ili kuongeza nafasi yao ya kufuzu kushiriki mtanange wa Ulaya msimu ujao. Ronaldo amesaliwa na mwaka mmoja kwenye mkataba wake na miamba wa Italia baada ya kujiunga nao akitokea Real Madrid mwaka 2018. Licha ya hatima ya Ronaldo kuyumba, kinara wa Juve Andrea Agnelli alifichua mpango wa klabu hiyo kurefusha mkataba wa fowadi huyo.