Mfuko wa kimataifa wa kulinda maslahi ya wanyama IFAW umesema umepata hekta 11,750 za ardhi huko Amboseli, kusini mwa Kenya kwa ajili ya uhifadhi wa wanyamapori.
Mwenyekiti wa Ranchi ya Kundi la Olgulului Ololarashi (OOGR) Bw. Daniel Leturesh, na mwenyekiti wa IFAW Bw. Azzedine Downes walisaini makubaliano yatakayowanufaisha wamiliki 3,598 wa ardhi kwa kodi ya ardhi na mapato ya utalii endapo ardhi yao iliandikishwa kisheria kama hifadhi ya wanyamapori.
Bw. Downes amehakikisha kuwa ardhi hiyo itaendelea kuwa mikononi mwa wamiliki wake na IFAW itashirikiana nao kuvutia wawekezaji kwenye sekta ya utalii miongoni mwa sekta nyingine ambazo zinatarajiwa kuleta fursa za kifedha kwa jumuiya hiyo, ili wasitegemee kupita kiasi sekta ya utalii, ambayo janga la Corona limeonesha kuwa inaweza kuvurugika.