Kazi ya kulinda makazi ya wanyamapori barani Afrika inatakiwa kuimarishwa ili kupunguza matishio yanayoletwa na mabadiliko ya tabia nchi, kupanuka kwa miji na kuongezeka kwa idadi ya watu.
Mwanakampeni wa wanyamapori Bibi Edith Kabesiime, wa ofisi ya Shirika la Kulinda Wanyama Duniani (WAP) kanda ya Afrika, amesema njia zenye uvumbuzi zinatakiwa ili kudhibiti kupungua kwa makazi ya wanyamapori barani Afrika na kuhimiza utalii.
Akiongea mjini Nairobi kwenye kongamano lililofanyika kwa njia ya video, Bibi Kabesiime amesema ni jambo muhimu kwa nchi za Afrika kutunga sheria zinazoimarisha ulinzi wa wanyama pori wanaokabiliwa na hatari mbalimbali.
Amesema kukabiliana na matishio matatu ya ikiolojia, uchafuzi wa hewa, mabadiliko ya tabia nchi na kupungua kwa bioanuai, kutakuwa na matokeo mazuri ya kulinda wanyamapori barani Afrika.