Matunda ya miaka mitano tangu ufanyike Mkutano wa Kwanza wa “Ukanda Mmoja, Njia Moja” yaliwa hadi na wananchi wa kawaida
2022-05-14 16:04:28| cri

Matunda ya miaka mitano tangu ufanyike Mkutano wa Kwanza wa “Ukanda Mmoja, Njia Moja” yaliwa hadi na wananchi wa kawaida

Pendekezo la “Ukanda Mmoja, Njia Moja” (BRI) lililotangazwa na rais wa China Xi Jinping mwaka 2013, kwa sasa linaonekana kuzaa matunda matamu kwa nchi zote zinazoshiriki kwenye pindekezo hili. Ukiwa sasa huu ni mwaka wa tano tangu Mkutano wake wa kwanza wa ushirikiano wa kimataifa ufanyike Mei 14-15, 2017, kuna mambo mengi sana ya kujivunia.

Tunafahamu kuwa pendekezo hili limejikita kwenye maeneo mbalimbali, ikiwemo miradi ya kiuchumi, kijamii na kiutamaduni. Lakini leo ningependa kuangalia zaidi upande wa utamaduni na mawasiliano kati ya watu, hasa kati ya watu wa China na Afrika. Hivi sasa pande hizi mbili zimeimarisha uhusiano na ushirikiano wa watu wa kawaida, chini ya nguzo kuu ya pendekezo la “Ukanda Mmoja, Njia Moja”. 

Mwingiliano wa utamaduni kati ya China na Afrika unaonekana kuwa mkubwa sana. Na hii ni kutokana na kwamba pande hizi mbili sasa zimekuwa zikifahamu baadhi ya tamaduni za kila upande. Utamaduni wa China umekuwa ukifahamika zaidi sasa, sio tu kwa mtu mmoja mmoja anayepata fursa ya kusafiri na kuja China kushuhudia kwa macho yake, bali hata kupitia tamthilia na filamu pia.

Pendekezo la “Ukanda Mmoja, Njia Moja” limefungua soko la burudani hasa tamthilia na filamu. Kupitia sekta hii China imeweza kutambulisha zaidi utamaduni wake kwa Waafrika, na kufanya watu wengi wa Afrika kuulewa kwa kina na hata kusema kwamba kuna baadhi ya desturi za China zinafanana sana na za Afrika. 

Hilda Malecela, ni Mtafsiri na Mtia Sauti wa Kampuni ya Startimes, yeye anasema kupitia kazi yake ameona kwenye suala la utamaduni kuna mambo mengi tu Wachina wanayofanana na Waafrika, na kutokana na kushabihiana huku, ndio maana mara tu tamthilia za Kichina zilipoingia Tanzania, Watanzania walizifurahia na kuzipenda sana. “Tunapozungumzia tamthilia ya Mao Doudou na mama mkwe wake, tamthilia ya kwanza kabisa ya Kichina iliyotafsiriwa kwa Kiswahili na kuoneshwa Afrika Mashariki, maisha yaliyoelezewa mle ni sawa na ya Mtanzania wa kawaida kabisa” alieleza Hilda.

Licha ya hayo, Hilda pia amegusia suala la mawasiliano, na kusema tangu kuanza kutekelezwa kwa Pendekezo la “Ukanda Mmoja, Njia Moja”, ambalo linawapatia fursa Waafrika kuja China na kutangamana zaidi na wenzao Wachina, mawasiliano yamekuwa mepesi sana. 

“Kwa kweli Wachina ni watu wakarimu sana na ni rahisi kuwasiliana nao. Nilipofika China kwa mara ya kwanza, nilikuwa sijui hata kusema asante kwa Kichina, lakini Wachina walijaribu kutumia kila njia ili tuweze kuwasiliana hata kwa kutumia lugha ya alama na ishara pia. Bahati nzuri wakati nafanya manunuzi dukani nikapata kila kitu ninachokihitaji, pia nimeweza kusafiri kwenye basi na subway bila matatizo yoyote. Aliongeza Hilda.

Ndani ya miaka mitano tangu ufanyike mkutano wa kwanza wa ushirikiano wa kimataifa wa Pendekezo la “Ukanda Mmoja, Njia Moja”, Wachina na Waafrika wanaona kuwa wamejengewa daraja imara kabisa. Abdul Maisala, ambaye ni Fundi Mitambo, Mtafsiri na Mtia Sauti kwenye kampuni ya Startimes, anasema kampuni yao imekuwa mstari wa mbele kutekeleza mipango yote ya kutangaza utamaduni wa pande zote mbili iliyoelekezwa kwenye pendekezo hili.

“Tunachokifanya hapa Startimes, tumekuwa kama daraja kati ya Wachina na Waafrika hasa wa nchi za Afrika Mashariki ambazo nyingi zinazungumza lugha ya Kiswahili. Tumekuwa tukiwaunganisha Waswahili wa Afrika Mashariki na Wachina”. 

Kampuni ya Startime pamoja na nyingine za China zinazojikita kutangaza tamthilia na filamu za China zimekuwa ni chachu katika kuwapa burudani Waafrika huku zikikuza mawasiliano na kuleta maelewano baina ya watu, na hasa kuongeza mwamko wa Wachina kupenda kujifunza lugha za Afrika.

“Wachina pia wana shauku kubwa sana ya kujifunza na kujua lugha ya Kiswahili na wengi wanazungumza Kiswahili fasaha kabisa. Kwa hiyo uwepo wetu na ufanyaji kazi wetu nchini China umeleta mchango mkubwa wa kuweza kuitambulisha Tanzania na Afrika Mashariki kwa Wachina.