Mwakilishi wa China katika UM asisitiza eneo la Sahel linatakiwa kutoa kipaumbele kwa maendeleo
2022-05-19 08:36:28| CRI

Mwakilishi wa kudumu wa China katika Umoja wa Mataifa Balozi Zhang Jun amesisitiza kuwa, eneo la Sahel barani Afrika linatakiwa kushikilia kutoa kipaumbele kwa maendeleo, huku likiongeza nguvu katika kupambana na ugaidi, na kuimarisha mshikamano na ushirikiano.

Balozi Zhang Jun amesema hayo alipotoa hotuba katika mkutano wa Baraza la Usalama la Umoja huo uliojadili suala la Sahel. Pia amesema, Afrika inakabiliwa na changamoto kubwa katika kutimiza maendeleo, na migogoro mbalimbali duniani katika sekta za chakula, nishati na fedha inaifanya hali ya Afrika kuzidi kuwa mbaya, haswa katika eneo la Sahel, ambapo watu zaidi ya milioni 10 wanakabiliana na uhaba wa chakula, na mamilioni ya watu wanakimbia makazi yao.  

Pia amesisitiza kuwa, eneo la Sahel linakabiliwa na hali mbaya ya ugaidi, na matukio ya kigaidi ya kuvuka mipaka ya nchi yanatokea mara kwa mara. Hivi sasa Umoja wa Mataifa unahimiza mchakato wa kufanya tathmini ya pamoja ya kimkakati na Umoja wa Afrika, Jumuiya ya Kiuchumi ya Nchi za Afrika Magharibi (ECOWAS), na nchi za Sahel. Amesema anatumai kuwa Umoja wa Mataifa utaimarisha mawasiliano na pande zote zinazohusika, na kutoa mpango wenye ufanisi wa ufumbuzi wa suala hilo.