Mkutano wa 14 wa kilele wa Nchi za BRICS utakaofanyika leo Juni 23 hapa Beijing umeifanya China ifuatiliwe na jumuiya ya kimataifa. Mtafiti wa Nigeria wa Taasisi ya Utafiti wa Afrika katika Chuo Kikuu cha Ualimu cha Zhejiang Dkt. Adekunle Osidipe alipohojiwa hivi karibuni na Shirika Kuu la Utangazaji la China CMG amesema, China ikiwa ni mwanzilishi wa kundi la BRICS, hakuna mashaka juu ya ahadi yake kwa dira na dhamira ya BRICS, na imetoa mchango muhimu katika kusukuma mbele ushirikiano halisi kati ya nchi za BRICS.
Kaulimbiu ya mkutano huo ni “kujenga uhusiano wa kiwenzi wenye ubora wa juu, na kuendeleza zama mpya ya maendeleo ya dunia”. Dkt. Osidipe anaona China ikiwa ni mwenyekiti wa zamu ya mwaka huu wa kundi la BRICS, itatumia fursa hii kukusanya nguvu kwa ajili ya maendeleo ya dunia. Amesema China siku zote inachukuliwa na nchi zinazoendelea kuwa mfano wa kuigwa kwenye nyanja ya maendeleo. Amesema nchi za BRICS kuweka mkazo katika ajenda ya maendeleo, kutumia manufaa yao linganishi na kuendelea kuimarisha ushirikiano wa kiutendaji, kutatia nguvu ya uhai kwenye mfumo wa BRICS katika dunia ya leo inayojaa sintofahamu, na pia kutaweka mfano mpya wa kuigwa kwenye shughuli za maendeleo ya dunia.
Miaka mitano iliyopita, China ilitoa pendekezo la utaratibu mpya wa ushirikiano wa “BRICS+” ili kuzinufaisha nchi nyingi zaidi katika kutafuta maendeleo ya kasi. Dkt. Osidipe amesema kati ya nchi wanachama wa BRICS, China ina sekta imara ya viwanda na uwezo mkubwa wa uzalishaji, Russia ni nchi inayouza ngano kwa wingi zaidi duniani, India ni hodari katika utengenezaji wa dawa, na Brazil na Afrika Kusini zina hazina kubwa ya madini, viumbe na maliasili. Anaona utaratibu wa “BRICS+” utazinufaisha nchi nyingi zaidi zinazoendelea kutokana na raslimali nyingi zilizonazo nchi za BRICS na matunda ya ushirikiano kati yao, na kuziongoza nchi zinazoendelea na hata dunia nzima kwenye njia ya kutimiza maendeleo.