Waziri wa Mambo ya Nje wa China apinga vikali kauli ya G7 juu ya suala la Taiwan
2022-08-05 09:08:18| CRI

Waziri wa Mambo ya Nje wa China Wang Yi jana Alhamis alipinga vikali kauli inayohusu Taiwan, ambayo imetolewa na mawaziri wa mambo ya nje wa Kundi la Nchi 7 (G7), akisisitiza kwamba imepotosha ukweli na kuchanganya mambo yaliyo sahihi na yasiyo sahihi.

Pingamizi hiyo ameitoa pembeni ya mikutano ya mawaziri wa mambo ya nje wa ushirikiano wa Asia Mashariki, akisisitiza kuwa masuala yote yanayohusiana na wasiwasi ulipo sasa juu ya suala la mlango bahari wa Taiwan yako wazi kabisa, na hata mambo yaliyo sahihi na yasiyo sahihi. Amesema Marekani ndio imeanzisha matatizo, imeleta mgogoro, na kundelea kuongeza taharuki.

Bw. Wang ameeleza kuwa uchokozi mkubwa uliofanywa na Marekani umeweka mfano mbaya, na kuhoji kwamba kama vitendo hivyo havitarekebishwa na kupingwa, kanuni ya kutoingilia mambo ya ndani itakuwepo? Sheria ya kimataifa bado itatekelezwa? Na amani ya kikanda itawezaje kulindwa?

Hivyo ameitaka jumuiya ya kimataifa kupinga vitendo vyovyote vinavyoichokonoa kanuni ya kuwepo kwa China moja, na vya kukiuka mamlaka ya nchi na ukamilifu wa ardhi wa nchi zote.