Viongozi wa G20 wasisitiza tena ahadi ya kushirikiana katika kukabiliana na changamoto za kiuchumi duniani
2022-11-17 09:05:29| CRI

Viongozi wa kundi la nchi 20 (G20) wamesisitiza tena ahadi yao ya kushirikiana katika kukabiliana na changamoto kubwa za kiuchumi duniani.

Kwenye azimio lililopitishwa mwishoni mwa mkutano wa 17 wa wakuu wa nchi za kundi la G20, viongozi hao wamesema watabeba jukumu kwa pamoja, na ushirikiano ni muhimu katika kufufua uchumi wa dunia, kukabiliana na changamoto na kuweka msingi wa ukuaji imara, endelevu, wenye uwiano na jumuishi. Pia wamesema ni muhimu kushikilia sheria ya kimataifa na mfumo wa pande nyingi utakaolinda amani na utulivu, na kusisitiza kuwa ufumbuzi wa migogoro kwa njia ya amani, juhudi za kukabiliana na misukosuko pamoja na diplomasia na mazungumzo ni muhimu.

Viongozi hao pia wamesema wamedhamiria kuzisaidia nchi zinazoendelea, hasa zenye maendeleo duni na nchi za visiwa zinazoendelea, katika kukabiliana na changamoto za dunia na kufikia Lengo la Maendeleo Endelevu.