Rais Xi atoa wito kwa China na Umoja wa Ulaya kuongeza mambo ya kuleta utulivu katika dunia yenye misukosuko
2022-04-01 21:18:39| cri

Rais Xi Jinping wa China amefanya mazungumzo kwa njia ya video na Mwenyekiti wa Baraza la Ulaya Bw. Charles Michel na Mwenyekiti wa kamati ya Ulaya Bibi Ursula von der Leyen.

Rais Xi amekumbusha kwamba miaka minane iliyopita alitoa pendekezo kwa China na Ulaya kuhimiza ushirikiano kati yao kwa ajili ya amani, ukuaji, mageuzi na ustaarabu, na mtazamo wa bado haujabadilika lakini kutokana na hali ya sasa umekuwa muhimu zaidi. Amesema China na Umoja wa Ulaya wana maslahi mapana ya pamoja na msingi thabiti wa ushirikiano.

Akibainisha uthabiti na mwendelezo wa sera ya China ya Umoja wa Ulaya, Rais Xi ametoa wito kwa Umoja wa Ulaya kuwa na mtazamo wake kuhusu China, kupitisha sera huru ya China, na kufanya kazi na China ili kukuza ukuaji thabiti na endelevu wa uhusiano kati ya China na Umoja wa Ulaya na kuongeza mambo yanayoletwa utulivu kwenye dunia yenye misukosuko.

Rais Xi amesisitiza kuwa, China na Umoja wa Ulaya zinapaswa kufanya kazi kama pande mbili kuu za kudumisha amani ya dunia, na kumaliza hali ya sintofahamu katika mazingira ya kimataifa kwa utulivu wa uhusiano kati ya China na Umoja wa Ulaya. Amesema Pande hizo mbili zinapaswa kuchukua nafasi ya mbele katika kulinda mfumo wa kimataifa ambao Umoja wa Mataifa ni msingi wake, utaratibu wa kimataifa wa unaoongozwa na sheria za kimataifa, na kanuni za kimsingi zinazosimamia uhusiano wa kimataifa kwa kuzingatia kanuni za Mkataba wa Umoja wa Mataifa, na kukataa kwa pamoja kuibuka kwa mawazo ya kambi kinzani na kupinga majaribio ya kurudi kwa vita mpya baridi, kwa nia ya kudumisha amani na utulivu duniani.

Rais Xi amedokeza kuwa China na EU zinapaswa kufanya kazi kama masoko mawili makubwa yanayokuza maendeleo ya pamoja, na kuimarisha mafungamano ya kiuchumi kwa ushirikiano wa wazi. Amesisitiza kuwa China itaendelea kujitolea kuimarisha mageuzi na kufungua mlango zaidi, na inakaribisha uwekezaji wa biashara wa Ulaya .

Bw. Michel na Bibi von der Leyen wamesema China ni nguvu muhimu duniani, na Umoja wa Ulaya unatilia maanani sana hadhi na majukumu ya China kimataifa, na kuendeleza uhusiano na China. Wamesema China na Umoja wa Ulaya zinafurahia uhusiano wa muda mrefu wa kunufaishana, na pande zote mbili zimejitolea kulinda amani na umoja wa pande nyingi. Wamesema katika hali ya sasa ya kimataifa, ni muhimu kwa Umoja wa Ulaya na China kuongeza mazungumzo na ushirikiano. Pia wameeleza kuwa tayari kuendelea kuimarisha ushirikiano na China katika nyanja kama vile uchumi, biashara, uwekezaji, nishati na maendeleo ya kijani, ili kukabiliana kwa pamoja changamoto za kimataifa kama vile COVID-19, mabadiliko ya tabianchi, ulinzi wa viumbe hai na kuhimiza amani ya dunia, ukuaji wa uchumi na ustawi wa pamoja.

Pande hizo mbili pia zimebadilishana maoni kuhusu hali ya Ukraine. Rais Xi amesisitiza kuwa China inasikitishwa kuona hali ya Ukraine imefikia hapa ilipo sasa, na msimamo wa China kuhusu suala la Ukraine ni thabiti na wa wazi. China daima inasimama upande wa amani na kufanya maamuzi kwa kujitegemea kwa kuzingatia sifa za kila jambo. Amesema China inataka kuzingatiwa sheria za kimataifa na kanuni zinazotambulika duniani kote zinazosimamia uhusiano wa kimataifa, kutenda kwa mujibu wa malengo na kanuni za Mkataba wa Umoja wa Mataifa, na kutetea usalama wa pamoja na ushirikiano na endelevu. Amesema China inaunga mkono juhudi za Umoja wa Ulaya kuelekea suluhu ya kisiasa ya mgogoro wa Ukraine, na imekuwa ikihimiza mazungumzo ya amani kwa njia yake. Amesisitia kuwa mazungumzo ya amani ndiyo njia pekee ya kuzuia kuongezeka kwa mivutano, na jumuiya ya kimataifa inapaswa kuweka mazingira mazuri kwa ajili ya mazungumzo kati ya Russia na Ukraine na kutoa nafasi kwa suluhisho la kisiasa.