Rais wa China aandika waraka katika vyombo vya habari vya Russia
2023-03-20 14:23:01| CRI

Waraka ulioandikwa na rais Xi Jinping wa China unaoitwa “Kuendelea na Ufunguaji wa Ukurasa Mpya wa Urafiki, Ushirikiano na Maendeleo ya Pamoja ya China na Russia” umechapishwa jumatatu katika gazeti la Russia na mtandao wa RIA Novosti, siku chache kabla ya ziara ya rais Xi nchini Russia.

Katika waraka huo, rais Xi amesema, Russia ilikuwa ni nchi ya kwanza kwake kufanya ziara baada ya kuchaguliwa kuwa rais wa China miaka 10 iliyopita, na katika mwongo mmoja uliopita, amefanya ziara nchini Russia mara nane, na katika kila ziara alikuwa na maatarajio makubwa na matokeo mazuri, na kufungua ukurasa mpya wa uhusiano wa China na Russia kwa pamoja na mwenzake wa Russia, Vladmir Putin.

Rais Xi amesema, ziara yake ijayo nchini Russia itakuwa ni safari ya urafiki, ushirikiano na Amani, na kwamba anatarajia kufanya kazi na rais Putin kwa pamoja kupitisha malengo mapya, mpango kazi mpya na hatua mpya kwa ajili ya ukuaji wa uhusiano wa uratibu wa kimkakati wa China na Russia katika miaka ijayo. Amesema ni muhimu kwa pande hizo mbili kuongeza kuaminiana na kutoa fursa zaidi za ushirikiano wa pande mbili ili kudumisha uhusiano wa China na Russia katika ngazi ya juu.

Akizungumzia mgogoro wa Ukraine, rais Xi amesema daima China imedumisha nafasi isiyo na upendeleo na haki kwa msingi wa suala husika, na imekuwa ikipendekeza mazungumzo ya amani. Amesema China imetoa mapendekezo kadhaa ikiwemo kushikilia malengo na kanuni za Mkataba wa Umoja wa Mataifa, kuunga mkono juhudi zote chanya za kutatua mgogoro huo kwa njia ya amani, na kuhakikisha utulivu wa mnyororo wa viwanda na ugavi duniani, mambo ambayo yamekuwa ni kanuni ya msingi kwa China katika kukabiliana na mgogoro wa Ukraine.