Afisa wa AU asema Afrika iko tayari kuwa na sarafu moja
2023-06-09 08:55:28| CRI

Afisa mkuu kutoka Umoja wa Afrika (AU) alisema Alhamisi kwamba chombo hicho kiko mbioni na mipango yake ya kuanzisha sarafu moja ya Afrika.

Katika hotuba yake aliyoitoa kwenye Mkutano wa 22 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Soko la Pamoja la Mashariki na Kusini mwa Afrika (COMESA), Kamishna wa Maendeleo ya Uchumi, Biashara, Utalii, Viwanda na Madini wa AU, Albert Muchanga, alisema viongozi wa nchi wanachama walipitisha vigezo vya muunganiko wa uchumi katika mwaka 2021 kama sehemu ya juhudi za kuwa na sarafu moja. Na kwamba vigezo hivyo vitatekelezwa na Taasisi ya Fedha ya Afrika ambayo makao yake makuu yatakuwa Nigeria.

Alibainisha kuwa Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) imekubali kuisaidia AU kukusanya rasilimali kwa ajili ya kuanzisha Taasisi ya Fedha ya Afrika.

Awali Rais wa Kenya William Ruto alielezea wasiwasi wake kuwa tofauti za sarafu zimekuwa kikwazo katika kukuza biashara barani Afrika.