Mapigano makali yaendelea kati ya jeshi la Sudan na kikosi cha RSF
2023-09-18 08:40:58| CRI

Mapigano makali yameendelea jumamosi kati ya Jeshi la Sudan na kikosi cha Mwitikio wa Haraka (RSF) katika maeneo mbalimbali ya mji mkuu wa nchi hiyo, Khartoum.

Vyombo vya habari vya huko vimesema, kikosi cha RSF kilifanya mashambulio makali yaliyolenga Kamandi Kuu ya Jeshi la Sudan katikati ya mji wa Khartoum na kambi nyingine za jeshi katika miji jirani ya Omdurman na Bahri.

Wakati mapigano kati ya Jeshi la Sudan na kikosi cha RSF yakiingia katika mwezi wa sita, kikosi cha RSF bado kinashikilia maeneo mengi ya mji wa Khartoum na maeneo mengine ya magharibi, huku Jeshi la Sudan likikalia maeneo makubwa ya kaskazini, mashariki na katikati ya nchi hiyo.

Takwimu zilizotolewa na Wizara ya Afya nchini Sudan zinaonyesha kuwa, tangu mapigano makali kati ya Jeshi la nchi hiyo na kikosi cha RSF mjini Khartoum na miji mingine kutokea April 15, watu 3,000 wameuawa na wengine zaidi ya 6,000 wamejeruhiwa.