Rais wa Tanzania kuhudhuria Maonesho ya Kimataifa ya Utalii ya Kiswahili
2023-10-04 08:44:03| CRI

Maonesho ya 7 ya Kimataifa ya Utalii ya Kiswahili (S!TE) yanayotarajiwa kufunguliwa baadaye wiki hii, yamevutia waoneshaji zaidi ya 200 na wanunuzi 150 wa kimataifa kutoka zaidi ya nchi 20 duniani.

Waziri wa Maliasili na Utalii, Angellah Kairuki amesema maonesho hayo yatakayoanza Ijumaa na kumalizika Jumapili yatafunguliwa rasmi na Rais Samia Suluhu Hassan jijini Dar es Salaam na kuongeza kuwa maonesho hayo kwa mara ya kwanza yatakuwa na bustani ya wanyama pori, wakiwemo simba, chui na fisi ili kuhimiza utalii wa ndani.

Akizindua maandalizi ya maonesho ya utalii Aprili 2023, Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Utalii Tanzania, Damasi Mfugale alisema maonesho hayo yatafuatiwa na safari za kufahamu mambo zaidi kwa muda wa siku sita katika vivutio mbalimbali nchini, vikiwemo Kilimanjaro, Mkomazi, Ruaha, Serengeti, magofu ya Kilwa Kisiwani na Songo Mnara, na Visiwa vya Zanzibar.

Mfugale aliongeza kuwa maonesho hayo yatahusisha shughuli kama vile maonesho ya biashara ya utalii, makongamano ya uwekezaji, semina na mitandao ya biashara.