Serikali ya Sudan yakataa rasimu ya azimio la UM linalopendekeza kamati ya uchunguzi
2023-10-05 09:06:22| CRI

Serikali ya Sudan imekataa rasimu ya azimio la Baraza la Haki za Binadamu la Umoja wa Mataifa (OHCHR) lililopendekeza kuunda kamati ya watu watatu ya uchunguzi kushughulikia ukiukaji na uhalifu wakati wa mzozo nchini Sudan.

Wizara ya Mambo ya Nje ya Sudan imethibitisha tena kukataa rasimu hiyo kwa sababu imesema sio sahihi kuelezea kile kinachotokea Sudan, na kwa sababu ina chuki dhidi ya Wanajeshi wa Sudan, na haizingatii vipaumbele vya kweli vya Sudan katika suala hili. Wizara hiyo iliongeza kuwa serikali imeweka kipaumbele cha juu katika haki za binadamu.

Wajumbe wa OHCHR kwa sasa wako katika majadiliano yanayoendelea mjini Geneva kuhusu rasimu ya azimio lililopendekezwa na Marekani, Uingereza, Norway na Ujerumani, ambayo inalenga kuanzisha kamati ya watu watatu ya uchunguzi kushughulikia ukiukaji na uhalifu wakati wa mzozo nchini Sudan. Nchi kadhaa, ikiwa ni pamoja na Saudi Arabia, zimechagua kutoidhinisha rasimu ya azimio hilo.