Wataalamu wa nyuklia wa Afrika wakutana nchini Kenya ili kuendeleza matumizi ya teknolojia kwa amani
2023-10-24 09:45:22| CRI

Mkutano wa nne wa Umoja wa Vijana wa Afrika kuhusu Nyuklia ulianza Jumatatu mjini Nairobi, Kenya, ambapo washiriki 2,500 wanahudhuria kujadili matumizi ya amani ya teknolojia ya nyuklia katika sekta mbalimbali na maendeleo ya utafiti.

Mkutano huo wa siku tatu umewaleta pamoja wadhibiti wa nyuklia, wasomi na wanafunzi kutoka zaidi ya nchi 20 za Afrika ili kutoa mikakati ya ushirikiano juu ya matumizi ya teknolojia ya nyuklia.

Katika hotuba yake ya ufunguzi, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Kudhibiti Nyuklia nchini Kenya, James Keter Chumba, alisema "Teknolojia ya nyuklia ni nzuri zaidi kwa uchunguzi wa magonjwa kama vile saratani kwa sababu haihitaji upasuaji na ni sahihi sana."

Alisema tiba ya mionzi ambayo hutumia teknolojia ya nyuklia pia ni chaguo la kutibu magonjwa magumu na sayansi ya nyuklia inaweza pia kusaidia wakulima kulinda mazao yao dhidi ya wadudu kwa kutumia mbinu za kuwafanya wadudu wawe tasa.

Naye Katibu Mtendaji wa Tume ya Afrika ya Nishati ya Nyuklia, Enobot Agboraw, amesema teknolojia ya nyuklia ni chanzo safi cha nishati ambacho kinaweza kusaidia kuongeza upatikanaji wa umeme kwa nchi za Afrika.