Polisi wa Afrika Kusini wateketeza dawa za kulevya zenye thamani ya dola milioni 42
2023-10-27 10:11:50| CRI

Mamlaka ya polisi ya Afrika Kusini imesema wameteketeza dawa za kulevya zenye thamani ya randi milioni 800 (kama dola milioni 42 za Kimarekani) Alhamisi mjini Johannesburg ili kuzuia zisiingizwe barabarani.

Kwa mujibu wa kamishna wa polisi wa kitaifa, Fannie Masemola, dawa hizo zikiwa ni pamoja na kokeini, heroini, mandrax na bangi, zilichomwa baada ya kupatikana wakati wa operesheni za kila siku za polisi nchini kote.

Masemola alifafanua kuwa dawa zote zilizokamatwa na polisi zilifanyiwa uchunguzi wa kitaalamu katika Maabara ya Polisi ya Sayansi ya Uchunguzi wa Jinai, na kesi zinazohusiana na dawa hizo zilimalizika na mahakama ilitowa amri ya kuziteketeza.

Jeshi la Polisi limesema limeteketeza tani 20.8 za dawa za kulevya zenye thamani ya randi bilioni 2 mitaani katika mwaka wa fedha 2022/2023.