Viongozi wa SADC wajadili kupeleka askari nchini DRC
2023-11-06 23:31:15| cri

Wakuu wa nchi wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) wamefanya mkutano maalum jumamosi iliyopita nchini Angola, ambapo walijadiliana masuala kadhaa ikiwemo kupeleka askari wake katika eneo la mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).

Mkutano huo ulioongozwa na rais wa Angola, Joao Manuel Lourenco, ulihudhuriwa na rais Felix Tshisekedi wa DRC, Samia Suluhu Hassan wa Tanzania, Cyril Ramaphosa wa Afrika Kusini, Hakainde Hichilema wa Zambia, na Emmerson Mnangagwa wa Zimbabwe.

Taarifa ya pamoja iliyotolewa baada ya mkutano huo imesema, viongozi hao wamerejea tena haja ya SADC ya kuongoza juhudi za kukusanya rasilimali ili kuwezesha Amani na usalama katika kanda ya SADC. Taarifa hiyo pia imesema juhudi hizo ni pamoja na kurejesha majadiliano ili kuanzisha na kutekeleza Mfuko wa Amani wa SADC na kushirikisha Wenzi wa Ushirikiano wa Kimataifa.