Juhudi na mchango mkubwa unaotolewa na watu wa kujitolea
2023-12-14 09:25:09| CRI

Siku ya Kimataifa ya Kujitolea huadhimishwa kila mwaka ifikapo Disemba 5. Hii ni siku iliyoteuliwa na Umoja wa Mataifa kusherehekea na kutambua michango ya wafanyakazi wa kujitolea duniani kote. Siku hii inatoa fursa ya kuongeza ufahamu kuhusu umuhimu wa kujitolea na kuwaheshimu watu binafsi na mashirika ambayo yanatoa muda na juhudi zao kuleta matokeo chanya katika jumuiya zao na kwingineko.

Mpango wa Umoja wa Mataifa wa Kujitolea (UNV) una jukumu muhimu katika kuendeleza na kuratibu Siku ya Kimataifa ya Kujitolea. Kila mwaka, kawaida kunakuwa na kaulimbiu au mwelekeo maalum wa siku hii, unaoangazia vipengele tofauti vya kazi ya kujitolea na athari zake kwa jamii. Kaulimbiu mara nyingi hulingana na malengo na masuala mapana ya maendeleo ya kimataifa. Na kaulimbiu yam waka huu ni “Kama kila mtu angefanya…”

Siku ya Kimataifa ya Kujitolea hutumika kama ukumbusho wa uwezo wa kujitolea kushughulikia changamoto, kuongeza ushirikishwaji wa kijamii, na kuchangia kwenye maendeleo endelevu. Siku hii pia inahimiza watu kutoka nyanja zote kujihusisha katika shughuli za kujitolea, iwe katika ngazi ya mashinani, kitaifa, au kimataifa, na kutambua uwezekano wa mabadiliko chanya yanayotokana na juhudi za pamoja za kujitolea.

Matukio, shughuli na kampeni mbalimbali hupangwa katika Siku ya Kimataifa ya Kujitolea ili kuonesha njia mbalimbali ambazo watu wa kujitolea wanachangia katika kujenga jumuiya imara na kukuza mshikamano wa kijamii. Pia ni siku ya kutoa shukrani kwa wanaojitolea na kuwatia moyo wengine kujiunga na harakati za kimataifa za kuchangia kwenye jamii kupitia hatua za kujitolea. Kwa hiyo kwa kuwa siku hii inamhusu kila mtu lakini zaidi vijana, leo kwenye ukumbi wa wanawake tutaangalia juhudi na mchango mkubwa unaotolewa na watu wa kujitolea.