Kikundi cha madaktari wa China chapongezwa kwa kuboresha huduma za afya nchini DRC
2024-01-31 08:32:56| CRI

Naibu waziri wa Afya wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo Bw. Serge Emmanuel Holenn amesema kikundi cha madaktari wa China kimesaidia kuboresha huduma za afya kwa watu nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).

Bw. Holenn ameyasema hayo kwenye hafla ya mapokezi iliyofanyika mjini Kinshasa kukaribisha kikundi cha 22 cha madaktari wa China waliowasili hivi karibuni, na kuaga kikundi cha 21 cha madaktari ambacho kitakamilisha kazi yake hivi karibuni.

Kwa niaba ya serikali ya DRC, Bw. Holenn alitoa shukrani zake za dhati kwa upande wa China kwa kutuma timu za madaktari nchini DRC kwa zaidi ya miaka 50, huku akitaja ushirikiano wa afya uliozaa matunda na unaoheshimiwa kati ya nchi hizo mbili.

Amekumbusha kuwa katika miaka ya hivi karibuni, madaktari wa China wamesaidia kushinda changamoto kama vile Ebola na janga la COVID-19, na kusaidia kulinda afya ya maelfu ya familia nchini DRC.