SGR ya Kenya yaongeza mabehewa mapya 50
2024-02-06 10:43:37| CRI

Huduma ya uchukuzi ya reli ya SGR imeongeza mabehewa mapya 50 ambayo yaliagizwa kutoka China, ili kuboresha ufanisi wa huduma za reli nchini humo na kusaidia kuhamisha mizigo kutoka barabarani, na kupunguza uharibifu unaosababishwa na malori makubwa.

Akisema kwenye taarifa iliyotolewa huko Mombasa, Kenya, Waziri wa Barabara na Uchukuzi Kipchumba Murkomen alisema kuwa mabehewa mapya ni sehemu ya mwitikio wa kimkakati wa Kenya kwa mienendo ya soko, na haja ya kukidhi mahitaji yanayobadilika kila wakati ya wateja na kuongeza makali ya ushindani katika kanda.

Alibainisha kuwa hii ni mara ya kwanza kwa mabehewa mapya kuongezwa tangu kuzinduliwa kwa SGR Mei 2017, na kwamba shehena ya pili ya mabehewa 250 kutoka China inatarajiwa kuwasili baadaye Februari nchini humo. Aliongeza kuwa mabehewa 20 kati ya yanayotarajiwa kuletwa yatakuwa na plagi za umeme ili kuwezesha usafirishaji wa makontena yaliyohifadhiwa kwenye jokofu, biashara ambayo haijawahi kutumiwa hadi sasa kwa SGR.