Tanzania yaandaa mkakati wa miaka mitano wa kuwalinda hwatu wenye ulemavu wa ngozi
2024-02-07 08:38:45| CRI

Serikali ya Tanzania imesema inaandaa mkakati wa miaka mitano unaolenga kulinda na kuboresha ustawi wa watu wenye ulemavu wa ngozi.

Maendeleo ya mkakati huo yametangazwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Kazi, Vijana, Ajira na Watu Wenye Ulemavu, Joyce Ndalichako, alipofanya mazungumzo na Mtaalamu huru wa Umoja wa Mataifa anayeshughulikia haki za watu wenye ulemavu wa ngozi, Muluka-Anne Miti-Drummond mjini Dodoma.

Ndalichako alimweleza mtaalamu huyo wa Umoja wa Mataifa kuwa mkakati huo unaoanzia mwaka 2024 hadi 2028 unahusu utoaji wa huduma za afya kwa watu wenye ulemavu wa ngozi, ulinzi wa haki zao na utoaji wa elimu.

Alisema mkakati huo wenye lengo kuu la kuondoa ubaguzi dhidi ya watu wenye ulemavu wa ngozi, umeandaliwa na Serikali kwa kushirikiana na Chama cha Watu wenye Ulemavu wa ngozi Tanzania (TAS) na wadau wengine.