Idadi ya vifo vya Wapalestina katika Ukanda wa Gaza yaongezeka hadi 29,692
2024-02-26 09:05:52| CRI

Wizara ya Afya ya Palestina inayoendeshwa na Hamas imesema, jeshi la Israel limewaua Wapalestina 86 na kuwajeruhi wengine 131 katika Ukanda wa Gaza katika saa 24 zilizopita, na kusababisha idadi ya vifo katika eneo hilo kuongezeka na kufikia 29,692 na majeruhi kufikia 69,979 tangu mgogoro kati ya Israel na Kundi la Hamas ulipotokea tarehe 7 Oktoba, 2023.

Wizara hiyo pia imesema waathirika wengi bado wako chini ya kifusi kutokana na mashambulizi makubwa ya mabomu, na ukosefu wa ulinzi wa raia na wafanyakazi wa uokoaji.

Vyanzo vya matibabu vya Palestina vimesema Mpalestina mmoja aliuawa na wengine wanne walijeruhiwa katika shambulizi la Israel dhidi ya nyumba moja kwenye eneo la Al-Shaaf, mashariki mwa mji wa Gaza.

Vyanzo hivyo pia vimeongeza kuwa mashambulizi ya makombora katika sehemu ya magharibi ya mji wa Khan Younis na eneo jirani la Al-Sabra la mji wa Gaza yamesababisha idadi kubwa ya vifo vya Wapalestina na wengine kadhaa kujeruhiwa.