Wataalamu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki wataka nchi wanachama kuhimiza ujasiriamali wa kidijitali
2024-03-11 08:43:22| CRI

Wataalamu kutoka Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) wamezitaka nchi wanachama wa jumuiya hiyo kuandaa na kutekeleza kanuni zinazohimiza ujasiriamali wa kidijitali.

Wito huo ulitolewa na Makao Makuu ya EAC kufuatia Mkutano wa Tatu wa Kikanda wa Sayansi, Teknolojia na Ubunifu (STl) wa jumuiya hiyo uliofanyika mjini Nairobi.

Wataalamu hao walisisitiza haja ya serikali kuweka mazingira mazuri kwa ajili ya wajasiriamali wa kidijitali kwa kuondoa ushuru na tozo kwa muda maalum, ili kuruhusu biashara hizi kujiimarisha. Pia wamehimiza vyuo vikuu na taasisi za mafunzo kuanzisha programu za kufundisha elimu ya mambo ya dijitali kuwalenga watu wa vijijini na mijini.

Katika sekta ya viwanda, wataalam walitetea kupitishwa kwa mbinu za teknolojia za kisasa kupitia matumizi ya mitambo ya kiotomatiki katika michakato ya uzalishaji.