Waasi wa M23 wateka miji karibu na Goma nchini DR Congo, juhudi za kutafuta amani zinaendelea
2024-03-13 08:42:40| CRI

Licha ya kuwepo kwa kikosi cha kikanda kutoka Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC) kilichotumwa kukabiliana na uasi, waasi wa M23 wameteka miji kadhaa ya kimkakati nje kidogo ya Goma, mji mkuu wa jimbo la Kivu Kaskazini mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).

Hatua iliyopigwa na M23 imezidisha mzozo wa kiusalama na kidiplomasia, huku nchi za kikanda zikiendeleza juhudi za kupanga mkutano kati ya viongozi wa Rwanda na DRC. DRC imeituhumu Rwanda kwa kuwaunga mkono waasi wa M23, tuhuma ambazo zilikataliwa na Rwanda na waasi wa M23. Kundi hilo la waasi, ambalo liliibuka tena mwishoni mwa 2021, limezusha migogoro na misukosuko ya kibinadamu na kuteka ngome kubwa katika ardhi ya DRC.

Kwa mujibu wa vyanzo vya kijeshi, waasi wa M23 wamedhibiti miji kadhaa inayozunguka Goma, kitovu cha kiuchumi, huku wakiliamuru jeshi la DRC (FARDC) kuondoa wanajeshi wake. Mji wa Vitshumbi, ulio katika mwambao wa Ziwa Edward, ndio wa karibuni zaidi kuangukia kwenye mikono ya waasi bila upinzani, ambapo wakazi wengi walikuwa tayari wamekimbia.