Ripoti: Uganda inalenga kuongeza mapato ya mwaka ya shughuli za utalii
2024-03-27 08:52:54| CRI

Mamlaka ya utalii ya Uganda imesema, nchi hiyo inatarajia kuongeza mapato ya mwaka ya shughuli za utalii  hadi kufikia dola bilioni 1.9 za kimarekani na kuongeza mapato kutoka kwa kila mtalii anayeingia nchini humo kutoka dola 1,052 hadi 1,500.

Waziri wa utalii, wanyamapori na mambo ya kale Bw. Tom Butime amesema hayo wakati akitangaza ripoti ya hali ya sekta ya utalii ya mwaka 2023.

Waziri huyo amesema mapato ya shughuli za utalii ya Uganda kwa mwaka 2023 yaliongezeka hadi kufikia zaidi ya dola bilioni 1 za kimarekani kutoka dola milioni 687 zilizoandikishwa mwaka 2022, ambazo alizitaja kuchangiwa na  juhudi kubwa za utangazaji wa utalii   zilizofanywa na wizara hiyo na wadau wengine.

Ripoti imeonesha kuwa mwaka 2023 idadi ya watalii kutoka nchi mbalimbali  ilifikia milioni 1.3, ikiongezeka kwa asilimia 56.5 ikilinganishwa na mwaka jana. Watalii kutoka nchi za Afrika wanaendelea kuchukua nafasi kubwa zaidi katika watalii wanaoingia nchini Uganda,  ilifikia kiwango cha asilimia 89.2.