Wapiganaji 81 wa al-Shabab wauawa katika operesheni ya jeshi la Somalia
2024-03-29 09:24:28| CRI

Jeshi la Somalia limewaua magaidi 81 wa kundi la al-Shabab katika operesheni ya siku tatu katika maeneo ya kati na kusini mwa nchi hiyo.

Wizara ya Habari, Utamaduni na Utalii ya Somalia imesema kwenye taarifa kwamba baadhi ya viongozi wa al-Shabab pia wameuawa katika operesheni hiyo iliyoanzia Jumatatu hadi Jumatano wiki hii katika majimbo ya Galmudug, Hirshabelle na Southwest.

Operesheni hiyo iliyoungwa mkono na washirika wa kimataifa inafuatia taarifa ya kijasusi ambayo ilisema kundi la al-Shabab lilikuwa linapanga kufanya shambulizi katika mji mmoja wa jimbo la Galmudug, katikati mwa Somalia.