Serikali ya Sudan yasitisha shughuli za vyombo vitatu vya habari vya Kiarabu
2024-04-03 09:27:25| CRI

Serikali ya Sudan imetangaza kusitisha shughuli za vyombo vya habari vya Al Arabiya, televisheni ya Al Hadath, na Shirika la Sky News Arabia nchini humo kutokana na ukosefu wa viwango vya kitaalamu na uwazi katika uandishi wa habari.

Kaimu Waziri wa Habari Graham Abdel-Qadir ametoa agizo la kusitisha matangazo ya vyombo hivyo mara moja, na kusisitiza kuwa uamuzi huo ni kwa ajili ya kulinda maslahi na maadili ya raia wa Sudan.

Machi 29, televisheni ya Sky News Arabia ilionyesha picha ya video ikidai kuhusika kwa wapiganaji wa kundi la IS wakishirikiana na Jeshi la Sudan (SAF), ripoti ambayo imekanushwa na serikali ya Sudan, huku Wizara ya Mambo ya Nje ya Sudan ikisema video hiyo si ya kitaaluma na yenye upendeleo.