WHO yatoa wito wa huduma ya afya kwa wote ili kukabiliana na mzigo wa magonjwa barani Afrika
2024-04-08 08:54:42| CRI

Mkurugenzi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) kanda ya Afrika, Matshidiso Moeti, amesema serikali za Afrika zinapaswa kuongeza  upatikanaji wa huduma bora ya afya kwa raia wote ili kupunguza mzigo wa magonjwa katika bara hilo.

Akizungumza jana wakati wa maadhimisho ya Siku ya Afya Duniani, Bi. Moeti amesema bara hilo linahitaji maamuzi ya kishujaa ya kisiasa, na mageuzi wa sheria na sera ili kutimiza ajenda ya huduma ya afya kwa wote.

Amesema kaulimbiu ya Siku ya Afya Duniani mwaka huu ni “Afya Yangu, Haki Yangu,” ikisisitiza haja ya serikali za nchi za Afrika kujumuisha upatikanaji wa huduma bora na nafuu za afya katika katiba zao.

Pia amezisifu serikali za Afrika kwa ahadi yao ya kufanyia marekebisho sera za afya na kuanzisha mipango ya bima ya kitaifa ya afya ili kupunguza maalipo kwa wagonjwa wanaohitaji huduma za afya.