Rais wa Kenya atoa wito wa maelewano wakati mgomo wa madaktari ukiendelea nchini humo
2024-04-08 08:54:08| CRI

Rais wa Kenya William Ruto amesema hakuna fedha za kuwalipa madaktari wanaoendelea na mgomo, wakati mgomo huo ukiingia katika wiki ya nne huku serikali na wahudumu wa afya wakishindwa kufikia makubaliano ya jinsi ya kumaliza mvutano huo.

Hata hivyo, rais Ruto ametoa wito kwa wahudumu wa afya kuelewa kuwa kuna ukomo kwa kiasi ambacho serikali inaweza kutumia katika mishahara yao na marupurupu yao mengine. Amesema serikali yake inathamini nafasi ya madaktari na madaktari walio katika mafunzo kwa vitendo katika sekta ya afya, na kuongeza kuwa, nchi hiyo haiwezi kuwa na matumizi yanayozidi uwezo wake.

Wahudumu wa afya walioanza mgomo wao wa kitaifa Machi 14, wanaitaka serikali kuajiri madakari wanaojifunza kwa vitendo katika kundi sahihi la kazi, kutekeleza nyongeza ya mishahara, kuwapatia bima kubwa ya afya, kuwalipia mafunzo yao baada ya kuhitimu, na kutoa ajira kwa zaidi ya madaktari 50,000 ambao hawana ajira.