Kampuni ya China yaanza ujenzi wa uwanja wa kisasa wa soka kaskazini mwa Tanzania
2024-04-08 08:53:31| CRI

Kampuni ya Ujenzi na Uhandisi wa Reli ya China (CRCEG) imeanza ujenzi wa uwanja wa kisasa wa soka mjini Arusha, kaskazini mwa Tanzania, ikiwa ni maandalizi ya mashindano ya fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) ya mwaka 2027.

Hafla ya uzinduzi wa ujenzi wa uwanja huo wenye ukubwa wa ekari 14.57 ilifanyika jumamosi iliyopita, ambapo maofisa wa ngazi ya juu wa serikali ya Tanzania waliungana na wahandisi na mafundi wa kampuni ya CRCEG walipoanza kujenga uwanja huo wenye uwezo wa kubeba watu 30,000.

Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo wa nchini Tanzania, Damas Ndumbaro, amesema ujenzi huo unaashiria hatua kubwa kwa kuwa Tanzania inajiandaa kuwa mwenyeji mwenza wa fainali za AFCON kwa kushirikiana na Kenya na Uganda.

Kwa upande wake, meneja wa mradi huo Gao Hongchun amesema, mhandisi amejipanga kujenga moja ya viwanja bora kabisa barani Afrika, kutoa ajira kwa wakazi wa huko, kuboresha ujenzi wa miji, na kuchochea maendeleo ya kiuchumi katika mkoa huo.