Maoni ya pamoja kati ya China na Ujerumani ni jibu lenye nguvu kwa “kelele” za nchi za Magharibi
2024-04-18 11:06:13| cri

Rais Xi Jinping wa China amekutana na Chansela wa Ujerumani Olaf Scholz tarehe 16, siku ya mwisho ya ziara yake nchini China, ambapo viongozi hao wawili walibadilishana maoni kuhusu uhusiano kati ya pande hizo mbili pamoja na masuala ya kimataifa na kikanda yanayofuatiliwa zaidi. China imeeleza kuwa, hakuna mgongano wa kimsingi wa maslahi kati ya China na Ujerumani, na kwamba ushirikiano wa kunufaishana kati ya pande hizo mbili si “hatari”, bali ni hakikisho kwa utulivu wa uhusiano kati ya nchi hizo mbili na fursa ya kujenga mustakabali. Kwa upande wake Ujerumani imeeleza nia yake ya kuendelea kuimarisha uhusiano kati yake na China, kukuza mazungumzo na ushirikiano katika sekta mbalimbali, na kuhimiza mawasiliano katika sekta za elimu na utamaduni, na inasisitiza kuwa hii ina umuhimu mkubwa kwa nchi zote mbili za Ujerumani na China hata dunia. Aidha pande hizo mbili zimeeleza kuunga mkono biashara huria na utandawazi wa kiuchumi duniani, na zingependa kukabiliana kwa pamoja na changamoto za dunia nzima, na kulinda amani na utulivu wa dunia.

Hayo yote yameonesha wazi kuwa, China na Ujerumani zina msimamo unaofanana katika masuala mengi muhimu, na zinaweza kushirikiana kuleta utulivu na uhakika zaidi kwa dunia.

Huu ni mwaka wa 10 tangu kuanzishwa kwa uhusiano wa kiwenzi na kimkakati kwa pande zote kati ya China na Ujerumani. Uhusiano kati ya nchi hizo mbili siku zote unatangulia mahusiano kati ya China na nchi kubwa za Magharibi. Viongozi wa pande hizo mbili kudumisha mawasiliano ya karibu, kuwa na utaratibu wenye ufanisi wa mazungumzo kati ya serikali za nchi hizo mbili, na kuwa na mazungumzo mbalimbali ya ngazi ya juu ya kimkakati na fedha, kumeweka msingi imara wa kudumisha ushirikiano wa uhusiano kati ya pande hizo mbili, na pia kuhimiza maendeleo yenye utulivu ya uhusiano kati ya China na Ulaya.

Ushirikiano kati ya China na Ujerumani unanufaishana pande zote mbili, na pia unaleta manufaa kwa dunia. Kadiri dunia inavyozidi kuwa na misukosuko mingi, ndivyo inakuwa muhimu zaidi kwa China na Ujerumani kuongeza Ustahimilivu na uhai wa uhusiano wao. Ushirikiano kati ya China na Ujerumani utatoa mchango mkubwa zaidi katika ushirikiano kati ya China na Ulaya, na pia utasaidia kuondoa “kelele” ambazo zinaharibu amani na maendeleo ya dunia.