Marais wa China na Ufaransa wafanya mazungumzo Paris
2024-05-07 09:10:24| CRI

Rais Xi Jinping wa China ambaye yuko ziarani nchini Ufaransa jana alasiri alifanya mazungumzo na mwenzake wa Ufaransa Emmanuel Macron mjini Paris.

Kwenye mazungumzo yao, Rais Xi amesema kuwa China inapenda kudumisha mawasiliano ya kimkakati na Ufaransa, kuheshimu maslahi makuu ya upande mwingine, na kuimarisha utulivu wa kimkakati katika uhusiano wa pande mbili. Pia nchi hizo mbili zinapaswa kuendeleza na kupanua wigo wa ushirikiano wa kunufaishana, na kuhimiza ukuaji na uwiano kwenye biashara ya pande mbili.

Kwa upande wake Rais Macron amesema, uhusiano kati ya Ufaransa na China una msingi imara, pande hizo mbili zinaheshimiana, zina maono ya mbali na zinaimarisha ushirikiano, hakika zitatoa mchango chanya katika kutatua changamoto zinazoikabili dunia na kuepusha makabiliano ya kikundi.

Viongozi hao wawili wametoa taarifa nne za pamoja kuhusu Hali ya Mashariki ya Kati, Akili Bandia na Usimamizi wa Dunia, Anuwai ya Viumbe na Bahari, na Mawasiliano na Ushirikiano wa Kilimo, na pia wamesaini nyaraka zipatazo 20 za ushirikiano zinazohusisha maendeleo ya kijani, usafiri wa anga, chakula na kilimo, biashara, utamaduni na kadhalika.