Wajumbe zaidi ya 600 kuhudhuria Mkutano wa 9 wa Idadi ya Watu wa Afrika utakaofanyika nchini Malawi
2024-05-20 08:54:41| CRI

Waziri wa Fedha na Uchumi wa Malawi Simplex Chithyola Banda ametangaza kuwa, wajumbe zaidi ya 600 kutoka Afrika wanatarajiwa kuhudhuria Mkutano wa 9 wa Idadi ya Watu wa Afrika, ambao umepangwa kufanyika kuanzia leo hadi ijumaa wiki hiiuu huko Lilongwe, mji mkuu wa nchi hiyo.

Waziri huyo amesema Malawi itanufaika sana na mkutano huo kutokana na kuwa utatoa jukwaa kwa nchi hiyo kuonesha nia yake ya kukabiliana na changamoto ya mwelekeo wa idadi ya watu.

Pia amesema mkutano huo utatoa jukwaa la kufanya majadiliano kuhusu sayansi, utafiti na siasa na mwelekeo wa idadi ya watu, na kwamba utasaidia kutafuta ufumbuzi wa changamoto zinazokabili mipango ya uchumi ya nchi hiyo.

Waziri wa Habari na Dijitali wa nchi hiyo Moses Kunkuyu ameema, nchi hiyo itatumia fursa za kiuchumi zitakazoletwa na mkutano huo, haswa katika sekta ya utalii na ustawi wa biashara ya ndani.