Wasomi wa China watoa wito wa kutafsiri “Makubaliano ya Dar es Salaam kati ya China na Afrika” kutoka nadharia hadi vitendo
2024-06-12 10:00:58| CRI

Katika mkutano wa Jukwaa la Jumuiya za Washauri Bingwa za China na Afrika uliofanyika hivi karibuni mjini Dar es Salaam, wasomi kutoka China na nchi 49 za Afrika walifikia “Makubaliano ya Dar es Salaam kati ya China na Afrika” , yanayotoa mashauri na mipango ya kutatua masuala na changamoto zinazoikabili dunia, makubaliano ambayo yamefuatiliwa na nchi nyingi na kuzusha mjadala kwenye jumuiya ya kimataifa. Katika kongamano la ngazi ya juu kuhusu makubaliano hayo lililofanyika Juni 7 mjini Beijing, wataalamu na wasomi wa China walioshiriki wote wameona kuwa, makubaliano hayo yana undani wa kina na umuhimu wa kivitendo.

Mkuu wa Taasisi ya Utafiti wa Afrika ya Chuo Kikuu cha Ualimu cha Zhejiang Profesa Liu Hongwu amesema, “Makubaliano ya Dar es Salaam kati ya China na Afrika” yametoa wito kwa jumuiya ya kimataifa kuendeleza ushirikiano, kusukuma mbele nchi mbalimbali kuelekea kwa pamoja kuwa za kisasa, na kujenga kwa pamoja Jumuiya ya Binadamu yenye Hatma ya Pamoja kwenye msingi wa kuheshimiana, kushikamana, kunufaishana na kustawi kwa pamoja. Mara baada ya makubaliano hayo kufikiwa na kutangazwa, yamepongezwa na nchi nyingi za Kusini kote duniani hasa nchi za Afrika. Amesema, makubaliano hayo ni matokeo ya asili yaliyopatikana kupitia mawasiliano na ushirikiano wa muda mrefu kati ya China na Afrika na kufunzana kati ya staarabu za pande hizo mbili, ambayo yamejumuisha hekima ya kiitikadi na mafanikio ya maarifa ya wasomi zaidi ya 5,000 kutoka karibu nchi 60 kupitia mawasiliano ya ana kwa ana katika miaka 15 iliyopita.

Wataalamu walioshiriki kwenye kongamano hilo wote wameona kuwa, makubaliano hayo yaliyofikiwa kati ya wasomi wa China na Afrika yameashiria kuinuka kwa mwamko wa kujiamulia na uwezo wa kujiendeleza wa nchi za Kusini mwa Dunia katika masuala ya kimataifa, na pia yameakisi kuwa nchi za Kusini mwa Dunia zinashirikiana kwa karibu zaidi katika kukabiliana na changamoto za pamoja zinazozikabili kwenye masuala ya maendeleo ya nchi na usimamizi wa dunia. 

Washiriki wa kongamano hilo wamekubali kwa kauli moja kuwa, makubaliano ya Dar es Salaam ni shirikishi na wazi, na yanahitaji kukamilishwa na kuboreshwa zaidi kutokana na mahitaji ya utekelezaji. Wametoa wito wa kutilia maanani ufanisi wa kueneza makubaliano hayo, na kubadilisha dhana ya makubaliano hayo kuwa mipango ya kiutendaji na miradi ya utekelezaji katika ngazi ya sera.