Waziri wa polisi wa Afrika Kusini asema kupunguza uhalifu wa kutumia nguvu ni kipaumbele
2024-07-17 08:43:30| CRI

Waziri wa Polisi wa Afrika Kusini Senzo Mchunu amesema kwamba kupunguza uhalifu wa kutumia nguvu, ukatili wa kijinsia, na mauaji ya wanawake bado ni moja ya vipaumbele vya juu vya idara ya polisi kwani kiwango cha uhalifu bado ni kikubwa sana nchini humo.

Mchunu amesema hayo wakati akitoa hotuba ya kupigiwa kura kwa bajeti ya Huduma ya Polisi ya Afrika Kusini (SAPS) katika Bunge la Kitaifa mjini Cape Town.

Ameongeza kuwa idara ya polisi itaendelea kupanua nguvu kazi yake ili kuongeza mwonekano wa polisi, kuboresha mwitikio wa jamii, na kujenga imani ya umma katika huduma ya polisi.

Mchunu amesema kuwa kuenea kwa silaha nchini Afrika Kusini kunahitaji umakini wa dharura na wa kujitolea, kwani mauaji mengi hufanywa kwa kutumia silaha zisizo halali. Akibainisha kuwa uhalifu umedhoofisha uchumi wa nchi hiyo, Mchunu ameahidi kwamba wataongeza juhudi za kukabiliana na uhalifu wa kupangwa, utakatishaji fedha na ufadhili wa ugaidi.