Serikali ya Kenya yataka maoni ya Wakenya kuhusu sheria ya Data
Serikali kupitia Wizara ya Teknolojia, Habari na Mawasiliano imewaomba Wakenya wajitokeze kuchangia kuhusu kubuniwa kwa kanuni mpya za kulinda data.
Katika ujumbe uliotumwa kwa vyombo vya mapema wiki hii, wizara hiyo ilieleza kuwa kanuni hizo zitawiana na Sheria ya Kulinda Data ya 2019, ambayo imetoa mwongozo kuhusu jinsi data ya mifumo ya kusajili wananchi inafaa kusimamiwa.
Data hiyo imehifadhiwa katika mfumo wa Huduma Namba, ambao unalenga kunasa taarifa za Wakenya, kwa dhamira ya mipango ya kifedha ya taifa hili. Watakaowasilisha maoni yao kupitia mjadala wanatakiwa kuhudhuria mjadala wa kitaifa kuhusu suala hilo jijini Nairobi na Mombasa na mjini Nakuru hapo Februari 27, 2020.
Watakaopenda kuandika maoni yao wanaombwa kutuma barua zao kwa Katibu katika wizara hiyo kabla ya Machi 2, 2020. Pia, wanaweza kuzituma kwa washirikishi wa kaunti, manaibu wao au kutuma baruapepe moja kwa moja kwa dataregulations@ict.go.ke.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |