Machar yupo DRC wasema Umoja wa Mataifa
Umoja wa Mataifa umesema Makamu wa Rais wa zamani wa Sudan Kusini Riek Machar ambaye alikuwa hajaonekana hadharani kwa muda yuko nchini Jamuhuri ya Kidemokrasia ya Congo.
Taarifa zainasema Kikosi cha Majeshi ya kulinda amani ya Umoja wa Mataifa yaliyopo Jamuhuri ya Kidemokrasia ya Kongo yalimsaidia yeye, mke wake pamoja na wengine kutoka kwenye mpaka unaogawa nchi hizo mbili. Rais wa Sudan Kusini Salva Kiir alimtimua kazi Bwana Machar mwezi uliopita baada ya mapigano baina ya majeshi yanayowaunga mkono na kusababisha maafa.
Taarifa zinasema Machar aliondoka Sudan Kusini kwa kuhofia usalama wake ikiwa ni siku chache baada ya kuzuka mapigano kati ya vikosi vyake na vile vinavyoitii serikali ya Juba. Msemaji wa Umoja wa Mataifa, Farah Haq, amesema Umoja wa Mataifa unatambua kuwa siku ya jumatano bwana Machar aliingia nchini Jamuhuri ya Kidemokrasia ya Congo kupitia mpaka baina ya Sudan Kusini na Jamuhuri ya Kidemokrasia ya Congo na kusaidiwa na majeshi ya Umoja wa Mataifa ya kulinda amani ambayo baadae walimsafirisha kwa ndege hadi mji mkuu Kinshasa.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |