Waliofariki ajali ya mlipuko wa lori la mafuta Tanzania yafikia 82
Ajali ya mlipuko wa lori la mafuta mjini Morogoro inaendelea kugharimu maisha ya watu na hivi sasa waliofariki kutokana na mkasa huo wa jumamosi asubuhi wamefikia 82.
Idadi hiyo imeongezeka baada ya majeruhi sita kati ya wale waliolazwa kwenye Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kuaga dunia, linaripoti gazeti la The Citizen.
Watu 62 walithibitishwa kufariki siku ya mkasa na zaidi ya 70 kujeruhiwa, na toka hapo idadi ya vifo imekuwa ikiongezeka taratibu.
Awali idadi ya majeruhi 46 walisafirishwa kutoka Morogoro mpaka Muhimbili kwa matibabu ya kibobezi.
Mpaka kufikia wiki hii, kwa mujibu wa Mkurugenzi wa Habari wa Muhimbili, Bw Amini Algaesha idadi ya majeruhi waliosalia hospitalini hapo ni 32, kati yao 17 wapo kwenye chumba cha wagonjwa mahututi.
Wengi wa majeruhi waliokimbizwa Muhimbili walikuwa wameunguzwa na moto kwa asilimia 80 na kuendelea.
Mkasa huo ulitokea majira ya saa mbili asubuhi ya Jumamosi baada ya lori lilibeba shehena ya petroli kuanguka katika mji wa Morogoro, na watu kuanza kuchota mafuta yaliyomwagika kisha mlipuko mkubwa kutokea.
Kumekuwa na hisia tofauti juu ya ajali hiyo lakini Rais wa nchi hiyo John Magufuli amewataka wananchi wake kuacha kuhukumu waliofariki na majeruhi.
© China Radio International.CRI. All Rights Reserved. 16A Shijingshan Road, Beijing, China. 100040 |