Wafanyakazi wa Idhaa ya Kiswahili ya CRI
China Radio International
China
Dunia
(GMT+08:00) 2004-08-03 16:47:52    
Tiba yake Kaburini

cri
    Bwana Tellya Wambwa wa Bongoma Kenya ametuletea barua akizungumzia ugonjwa wa ukimwi, pamoja na maoni yake kuna shairi kuhusu ukimwi, anasema angeomba wakuu wa Radio China Kimataifa walichapishe shairi hili katika tovuti (www.cri.cn) kwa lugha tofautitofauti kama vile kingereza, kijapani, kihispaniola, kitaliano, kihindi, kijerumani pamoja na lugha nyingine ili kuwaelimisha watu wasio na virusi vya ukimwi duniani kote. Shairi alilotuletea Bw Wambwa lina kichwa kisemacho " TIBA YAKE KABURINI" na maelezo ya shairi hilo yanasema:

      Nalalama ukumbini, ugonjwa hata sana

      Ukimwi wapenya ndani, kwa kweli raha hatuna

      Tuko na wasiwasi, sote makini hatuna

      Ukimwi dawa hauna, tiba yake kaburini.

      Siji kuwashitueni, bali ukweli kunena

      Sababu ndugu zangu, shida imepatikana

      Hatuwezi asilani, kuanza kudanganyana

      Ukimwi dawa hauna, tiba yake kaburini

      Tulikotoka jamani, hata fununu hatuna

      Kuutambua mwilini, pia ni vigumu sana

      Mapema hujulikani, na matibabu hauna

      Ukimwi dawa hauna, tiba yake kaburini

      Huu ugonjwa jamani, huruma kamwe hauna

      Waupata tu rahani, na bila kujua tena

      Au kwa matibabuni, huenda ukapatikana

      Ukimwi dawa hauna, tiba yake kaburini

      Hamu ya kula huoni, hapo ukimwi washona

      Wabadilika mwilini, kijivu kuonekana

      Kisha wakonda mwili, halafu wakaukiana

      Ukimwi dawa hauna, tiba yake kaburini

      Nidhamu tuidhamini, kwa wapenzi sana sana

      Jua mmoja mwandani, halafu tujependana

      Hamu isituzidini, na yeyote kulalama

      Ukimwi dawa hauna, tiba yake kaburini

      Tokeni uasherati, kwani huo si ungwana

      Uasherati ndo soko, la ukimwi kufanana

      Tusijiuze mwilini, pasi hata kupendana

      Ukimwi dawa hauna, tiba yake kaburini

      Tuendapo matemboni, tusilewe tu bayana

      Kuonana kimwili, na yeyote toneana

      Hapa twende hatarini, kwa tendo kujamiiana

      Ukimwi dawa hauna, tiba yake kaburini

      Huko hospitalini, mtufikirie tena

      Sindano mtudungeni, zilizosafishika sana

      Kwani hasipitalini, eti unambukizana

      Ukimwi dawa hauna, tiba yake kaburini

      Kwa sasa twawaombeni, waaguzi kupambana,

      Madaktari jaribuni, dawa ije patikana,

      Hata dawa ya shambani, ikiwa yawezekana

      Ukimwi dawa hauna, tiba yake kaburini

      Tukishindwa wenzanguni, hapo tukipatikana

      Tusihamaki lakini, kuanza gawagawana

      Wenzetu twafikirini, tusiage na laana

      Ukimwi dawa hauna, tiba yake kaburini

      Ninakoma ukingoni, na ujumbe wangu tena

      Wasiwasi tuondoeni, kwani haina maana

      Lililoko tujikingeni, ushikwapo shikamana

      Ukimwi dawa hauna, tiba yake kaburini

   Bwana Telly Wambwa anasema, ana matumaini kuwa tutalifurahia shairi lake kuhusu ukimwi. Shairi hili ni kama marudio kwani kuna wakati fulani alituma shairi hili la ukimwi kwa Radio China Kimataifa. Lakini hata hivyo tunashukuru kwa Shairi hili ambalo limeweza kuwakumbusha watu hatari ya Ugonjwa wa Ukimwi. Lakini tusikate tamaa, kwani wataalamu wanafanya utafiti na kutengeneza dawa mpya za kutibu ugonjwa wa ukimwi.

Idhaa ya Kiswahili 2004-08-03