Wafanyakazi wa Idhaa ya Kiswahili ya CRI
China Radio International
China
Dunia
(GMT+08:00) 2004-08-31 09:43:43    
Makabila madogomadogo ya China yanayopewa haki ya kujiendesha (sehemu A)

cri
    China ni nchi yenye makabila mengi. Miongoni mwa idadi ya watu bilioni 1.3 nchini China, watu wa Kabila la Han ni wengi kabisa ambao wanachukua asilimia 91. Mbali na kabila la Han, pia kuna makabila mengine 55 nchini China. Idadi yote ya watu wa makabila hayo inachukua asilimia 9 ya idadi ya jumla ya watu wa China. Ndiyo maana, makabila hayo 55 yanaitwa makabila madogomadogo. Sasa tunawaletea makala ya tatu ya chemsha bongo kuhusu miaka 55 ya China mpya, ambayo itawafahamisha hali ya jumla ya maisha na maendeleo ya watu wa makabila madogomadogo nchini China.

    Kabila la watibet ni moja ya makabila 55 madogomadogo nchini China. Mnayosikia ni matangazo ya lugha ya kitibet yaliyorekodiwa na mwandishi wetu wa habari alipotembelea

    mkoa unaojiendesha wa Tibet, China. Ukiwa Tibet, ukifungua redio, utasikia matangazo ya lugha ya kitibet; ukifungua televisheni utatazama vipindi vya lugha ya kitibet; ukiingia katika shule za msingi, utasikia watoto wanaosoma kwa lugha ya kitibet; ukitembea barabarani, utaona mabango ya milangoni yaliyoandikwa kwa lugha ya kitibet na ya kihan yaani lugha ya kichina.

    Kwa kweli katika sehemu nyingine zote wanakoishi watu wa makabila madogomadogo nchini China, utaona hali kama hiyo na kusikia watu wa makabila mbalimbali wakiongea kwa lugha zao wenyewe.

    Katika miaka 55 iliyopita tangu kuanzishwa kwa Jamhuri ya watu wa China, serikali ya China siku zote inafuata sera ya usawa, mshikamano na usitawi wa pamoja wa makabila yote, na kutekeleza mfumo wa kujiendesha katika sehemu mbalimbali wanakoishi watu wa makabila madogomadogo. Kati ya mikoa 34 ya China, mikoa mitano ni sehemu zinazojiendesha za makabila madogomadogo, kama vile wamongolia, waurgur, wahui, wazhuan na watibet.

    Mbali na mikoa hiyo inayojiendesha, China imeweka tarafa au wilaya nyingi zinazojiendesha za watu wa makabila madogomadogo. Watu hao wanajiendesha katika sehemu mbalimbali kadiri ipasavyo. Hivi sasa eneo la kujiendesha kwa makabila madogomadogo limefikia zaidi ya nusu ya eneo la jumla la nchi ya China.

    Katiba ya China inasema kuwa, China itafuata utaratibu wa kujiendesha kwa makabila madogomadogo. Utaratibu huo ulianza kutekelezwa kuanzia siku ya kuzaliwa kwa Jamhuri ya watu wa China. Ilipofika miaka ya 80 ya karne iliyopita, China ilibuni "Sheria ya kujiendesha kwa sehemu za makabila madogomadogo", katika hali ambayo ujenzi wa utaratibu wa kisheria utasukumwa kote nchini China. Hivyo utaratibu wa kujiendesha kwa sehemu za makabila madogomadogo ulithibitishwa kwa sheria maalum, na kuongezwa kanuni nyingi halisi kuhusu mamlaka ya kujiendesha.

Idhaa ya kiswahili 2004-08-31