Wafanyakazi wa Idhaa ya Kiswahili ya CRI
China Radio International
China
Dunia
(GMT+08:00) 2005-05-10 11:17:25    
Barua 0503

cri
Kabla ya kuwaletea barua tulizozipokea, tunapenda kuwaarifu wasikilizaji wetu kuwa, toleo la kwanza la jarida dogo la Daraja la Urafiki mlilokuwa mkilisubiri kwa hamu limeshapishwa na litaanza kutolewa wiki ijayo. Baada ya siku chache zijazo, tutawatumia wasikilizaji wetu wengi jarida hilo. Kwenye toleo la kwanza la jarida hilo tumechapisha risala ya mwaka mpya aliyoitoa mkuu mpya wa Radio China kimataifa Bwana Wang Gennian, barua, makala na mashairi tuliyopokea kutoka kwa wasikilizaji wetu na makala chache zinazojulisha utamaduni na vivutio nchini China.

Kutokana na uzoefu wetu mdogo, kutakuwepo na dosari kidogo kwenye toleo la kwanza la jarida hilo, na huenda lisiwavutie wasikilizaji wetu kama tunavyotaka. Tunawaomba wasikilizaji wetu watakaotumiwa jarida hilo, watuvumilie kwa hilo na wawe tayari kutoa maoni na mapendekezo yao. Polepole ndio mwendo, tuna imani kuwa, kutokana na juhudi za pamoja za wasikilizaji wetu, tutaweza kuboresha siku hadi siku jarida hilo ili liwavutie na kuwafurahisha wasikilizaji wetu na kuwa daraja halisi la urafiki kati ya Radio China kimataifa na wasikilizaji wake.

Msikilizaji Yohana Lulyalya Sayii wa sanduku la posta 116 Ng'wang'wali Bariadi Tanzania ametuletea barua akisema kuwa, anashukuru sana kwa radio China Kimataifa kuwapatia wasikilizaji fursa ya kutoa maoni na mapendekezo kuhusu kuboresha vipindi mbalimbali vya idhaa ya kiswahili ya Radio China kimataifa, hasa kuhusu jarida la Daraja la Urafiki.

Yeye anaunga mkono kwa kufanikisha mambo mengi ambayo watazidi kupendekeza katika jarida letu. Na ametuletea shairi lenye sehemu mbili, sehemu ya kwanza inahusu lugha na ya pili inahusu urafiki. Pia anaomba kuwe na jopo ambalo litashughulikia na kuboresha maswala mbalimbali katika jarida la Daraja la Urafiki.

Yeye Yohana Lulyalya Sayii anajipendekeza awemo katika jopo hilo ili kuboresha jarida hilo, kwa kuchangia mambo mbalimbali ambayo yatakuwa na mvuto kwa wasomaji wa jarida hilo duniani, kwani idhaa hii haina ubaguzi. Na anaitakia Radio China kimataifa izidi kupasua mawimbi ulimwenguni kote hadi sayari ya mwisho.

Shairi lake linasema hivi:

Lugha hii ni ya mbele, idhaa nyingi hutangaza

Walakini pole pole, wasomi nao huhimiza

Kitu ubora milele, lugha hii kuhimiza

Nakufikia kileleni, ni CRI yatangaza

Tudumishe urafiki, kwa lugha yetu kiungo

Kiswahili kina sifa, kwa nahau na maana

Huyafanya mataifa, mengi kusikilizana

Kikitoa taarifa, kwa wengi huwa bayana

Tena kinaleta sifa, kwa kuitangaza China

Tudumishe urafiki, kwa lugha yetu kiungo

Urafiki jambo zuri, vitu vyote huungika

Chemchem husafiri, kutafuta ushirika

Mto mwenziwe bahari, kiangazi kwa masika

Mchina mie fahari, urafiki kuuweka

Akutakaye mtake, vibaya kumuacha

Nami sina makeke, kwa jambo ninalotaka

Natamani nifike, kukomaza ushirika

Mkono wako nishike kama ulivyo tunuka

Nimesoma na shairi, katika wako waraka

Sikuona dosari, hata mwisho nikafika

tungo yako ni nzuri, inapaswa kusifika

Urafiki ni mzuri, mambo mengi kusifika

Msikilizaji wetu Wallace Masanja wa sanduku la posta 85 Sikonge Tabora Tanzania anasema katika barua yake kuwa, yeye ni miongoni mwa wasikilizaji wa Radio China kimataifa inayowarushia matangazo kutoka Beijing kwa kupitia masafa mafupi. Anapenda kutoa mapendekezo yake juu ya uandaaji wa jarida dogo la Daraja la Urafiki. Mapendekezo yake ni kama yafuatayo:

Kwanza anaomba jarida la daraja la urafiki liwe tayari kupokea maswali mbalimbali kutoka kwa wasikilizaji wetu, na baadaye kujibiwa nasi katika toleo linalofuata. Kwani kwa kufanya hivyo itawasaidia wasikilizaji wote wanaoishi katika dunia ya tatu kuweza kufahamu mambo mbalimbali, kwani yeye ni mmoja wapo anayependa kutambua ni jinsi gani ulimwengu unavyokwenda.

Pili anaomba katika uandaaji wa gazeti dogo la daraja la urafiki liwe na sehemu maalum itakayowapa wasikilizaji nafasi ya kuweza kutuma salamu kupitia gazeti hilo. Kwani kwa kufanya hivyo ndugu watangazaji wataweza kuongeza wasikilizaji wa CRI. Hayo ndio mapendekezo yake katika uandaaji wa gazeti dogo la daraja la urafiki.

Tunaona mapendekezo yake yote ni mazuri ambayo yatasaidia kazi yetu ya kuhariri na kuchapisha gazeti letu dogo la daraja la urafiki, tunamshukuru sana. Ni matumaini yetu kuwa wasikilizaji wetu watatuletea maoni na mapendekezo baada ya kusikiliza matangazo, kutembelea kwenye tovuti na mengineyo.

Na msikilizaji wetu Hilal Nasor Zahor Al Kindy wa sanduku la posta 119 Al Amrat Oman, ametuletea barua akisema kuwa, anashukuru iwapo tutachapisha shairi lake hilo kwenye jarida dogo la daraja la urafiki, shairi lake hilo lina kichwa kinachohusu Maji

Hakika maji yakiadimika binadamu ana taabu

Mungu katupa riziki yake kwetu

Kila kitu kinahitaji maji sana

Bila ya maji maisha yana taabu

Mwili wa binadamu ni kiasi cha 75 % ya maji

Maji lazima tuyahifadhi sana

Maji pia yahitajiwa na ndege na miti

Nyumba huwezi kujenga bila ya maji

Tena maji yahitajiwa kwa mwili

wa binadamu na wanyama

Kwa hiyo nawaomba wote tuyatunze

na tuyatumie kwa manufaa

Tunamshukuru sana kwa shairi lake hilo linalowaonya watu wa dunia nzima wathamini maji ambayo ni kitu kisichoweza kukosekana katika maisha ya watu na uzalishaji mali.

Idhaa ya kiswahili 2005-05-10