Wafanyakazi wa Idhaa ya Kiswahili ya CRI
China Radio International
China
Dunia
(GMT+08:00) 2007-01-22 19:23:49    
Uzalishaji kwenye sekta ya utamaduni nchini China waendelea kwa kina

cri

Kongamano la nne kuhusu uzalishaji kwenye sekta ya utamaduni ulimalizika siku chache zilizopita mjini Beijing. Wajumbe kutoka idara za serikali, makampuni na idara za watafiti zaidi ya mia moja walihudhuria kongamano hilo na kujadili kwa kina kuhusu maendeleo ya uzalishaji katika sekta ya utamaduni nchini China.

Uzaishaji katika sekta ya utamaduni umepata maendeleo ya haraka tokea mwaka 2000, na kutokana na sera nzuri za serikali makampuni husika yamestawi haraka. Mchango wa uzalishaji katika sekta ya utamaduni kwa pato la taifa unaongezeka.

Kongamano hilo lilianza mwaka 2003, na linafanyika kila mwaka, lengo la kongamano hilo ni kutoa mwongozo wa kuelekeza maendeleo ya uzalishaji katika sekta ya utamaduni na kuwaletea watu husika fursa ya kubalishana uzoefu. Mada za kongamano hilo zikiwa ni pamoja na kuandaa watu wa wanaoshughulikia uzalishaji katika sekta ya utamaduni, hali ya maendeleo ya kisehemu, kuwekeza na kuchangisha fedha kwa ajili ya uzalishaji huo. Naibu mkurugenzi wa idara ya taifa ya uvumbuzi na maendeleo ya uzalishaji katika sekta ya utamaduni Prof. Chen Shaofeng alipozugumza na waandishi wa habari alisema, hivi sasa nchini China kumetokea hamasa kwenye uzalishaji wa shughuli za utamaduni, lakini shughuli hizo zikiendeshwa bila umakini hamasa hiyo itapungua haraka kama povu la sabuni. Alisema,

"Nashauri kwamba serikali za mitaa zinapopanga maendeleo ya uzalishaji katika sekta ya utamaduni zinapaswa zishirikiane na makampuni na idara za watafiti, ili zipate kianzio cha kuendeleza maendeleo endelevu ya uzalishaji huo ili kukwepa hamasa inayotokea kwa ghafla na kupotea haraka."

Katika miaka ya karibuni, uzalishaji katika sekta ya utamaduni umepata maendeleo makubwa, hapo mwanzo aina moja moja ya utamaduni ilisukuma maendeleo ya aina nyingi za utamaduni. Kwa mfano, mkoa wa Yunnan, ambapo kuna aina nyingi za utamaduni wa kikabila, mchezaji mashuhuri wa dansi duniani Bi. Yang Liping alihariri mchezo wa nyimbo na dansi uitwao "Uzuri wa Mkoa wa Yunnan" kwa mujibu wa mila na desturi za makabila tofauti. Tokea mwaka 2004 mchezo huo umeoneshwa mara mia kadhaa huku na huko nchini China na mara karibu elfu moja katika nchi za nje. Mchezo huo umesukuma kwa nguvu maendeleo ya uzalishaji katika sekta ya utamaduni mkoani humo.

Kadhalika mkoani Guizhou pia kuna makabila mengi, ofisa mwandamizi wa mkoa huo alisema, uzoefu wa mkoa wa Yunnan pia unafaa kwa mkoa huo. Kwenye kongamano hilo alisema,

"Mkoani Guizhou kuna makabila 17, na kuna aina nyingi za utamaduni. Kutokana na historia tofauti, watu wa makabila hayo madogo madogo pia wanaishi kwa kufuata mila na desturi tofauti, na vile vile wanatofautiana katika mapambo ya mavazi, lugha, chakula, mila ya ndoa, nyimbo na ngoma, na ingawa wanaishi maisha ya hivi leo lakini wanaendelea na tabia na desturi za kiasili ambazo zina thamani kubwa kiutamaduni."

Utamaduni kama huo wa kisehemu ni moja ya mada zilizojadiliwa sana katika kongamano hilo. Wataalam wanaona kuwa kustawisha uzalishaji wa aina hizo za utamaduni sio tu kunahitaji wahariri wa michezo bali pia kunahitaji maofisa mahsusi wanaoshughulikia mambo ya utamaduni huo. Naibu mkuu wa taasisi ya utafiti wa uzalishaji katika sekta ya utamaduni katika Chuo Kikuu cha Beijing Bw. Xiang Yong alisema, kuandaa maofisa mahsusi wa utamaduni ni muhimu sana kwa ajili ya kuendeleza uzalishaji katika sekta ya utamaduni. Alisema,

"Tunapoandaa mpango wa kuendeleza uzalishaji katika sekta ya utamaduni, kitu cha kwanza ni kuwaelimisha maofisa wa utamaduni wawe na ufahamu tofauti na ule wa zamani kuhusu utamaduni wa kawaida."

Hivi sasa thamani ya uzalishaji katika sekta ya utamaduni nchini China bado haijafikia 3% ya pato la taifa, kiasi hicho ni kidogo sana ikilinganishwa na nchi zilizoendelea, kwa hiyo uzalishaji huo una nafasi kubwa ya kuendelea. Mwaka 2006 thamani ya uzalishaji huo iliongezeka kwa asilimia 10 ikilinganishwa na mwaka uliotangulia. Naibu mkurugenzi wa idara ya taifa ya uvumbuzi na maendeleo ya uzalishaji katika sekta ya utamaduni Prof. Chen Shaofeng alisema,

"Kwa sababu uwekezaji katika sekta hiyo una hatari yake, kwa hiyo mikopo au uchangishaji wa kawaida wa fedha haufai kwa sekta hiyo, tunashauri Benki ya Maendeleo itenge kiasi cha fedha kuunga mkono uzalishaji huo, lakini kufanya hivyo kunahitaji kuungwa mkono na sera za serikali."

Prof. Chen Shaofeng alisema, miezi kadhaa iliyopita, serikali ya China ilitangaza programu ya maendeleo ya miaka mitano ya utamaduni, na imesisitiza kuendeleza haraka uzalishaji katika sekta ya utamaduni. Ana uhakika kwamba katika miaka kadhaa ijayo uzalishaji huo hakika utapata maendeleo makubwa na yatatokea mashirika makubwa.

Idhaa ya kiswahili 2007-01-22