Wafanyakazi wa Idhaa ya Kiswahili ya CRI
China Radio International
China
Dunia
(GMT+08:00) 2008-02-27 16:51:49    
Maisha bora ya watu wa kabila la Wakazakh kwenye makazi ya kudumu

cri
Kwenye sehemu ya kaskazini ya mkoa unaojiendesha wa kabila la Wauyghur wa Xinjiang, kuna kabila la Wakazakh ambalo ni kabila la ufugaji lenye historia ndefu sana. Zamani mahema ya muda, nguo mbovu zilizotengenezwa na ngozi ya mbuzi zilikuwa dalili ya maisha ya wafugaji wa kabila la Wakazakh waliokuwa wakihama hama mara kwa mara, lakini sasa baadhi yao wameweka makazi ya kudumu, na kuanza kuishi maisha ya kisasa. Leo tutawaletea maelezo kuhusu maisha mapya ya familia moja ya kabila la Wakazakh.

Bw. Adelhan ni mzee wa kabila la Wakazakh, anaishi pamoja na mke wake na watoto wanne kweye kijiji cha Sakru ya wilaya ya Fuhai mkoani Xinjiang. Nyumba yao yenye eneo la mita za mraba 116 ilijengwa kwa matofali. Lakini katika miaka kadhaa iliyopita, maisha yao hayakuwa ni hivyo, Bw. Adelhan alisema,

"Zamani wakati wa siku za joto tuliishi kwenye mbuga ya mlima wa Altai, na wakati wa siku za baridi tulihamia mliama wa Shaur ili kuwafuga mifugo. Safari ilikuwa ndefu na mifugo ilikuwa wengi. Tuliishi kwenye hema ya Huosi na kutumia taa za mafuta, kwa kuwa hatukuwa na umeme."

Huosi ni hema rahisi ndogo inayotumiwa na watu wa kabila la Wakazakh. Ndani yake kuna eneo ndogo, na haiwezi kuzuia baridi. Wakati siku za baridi zilipowadia, maisha ya familia ya Bw. Adelhan huwa magumu zaidi. Alisema,

"Hata nguo ya ngozi ya mbuzi haiwezi kukinga baridi. Wakati maafa ya theluji yalipotokea, mamia ya mifugo wetu walikufa."

Ili kukabiliana na maafa ya theluji, familia ya Bw. Adelhan na familia ngingine 30 za wafugaji zilishirikiana kujenga nyumba kwa udongo na miti kwenye mabonde kati ya milima ya Altai na Shaur. Ingawa nyumba ilikuwa nzuri kuliko zamani, lakini maisha bado yalikuwa magumu, kutokana na wingi wa kupita kiasi wa mifugo, nyansi zilipungua kwa haraka.

Mwaka 2005, ili kuwasaidia wafugaji kuongeza mapato na kuboresha maisha, serikali ya wilaya ya Fuhai ilianzisha mradi wa kuwapangia makazi ya kudumu. Baada ya mwaka mmoja, kijiji kipya ya Sakru kilianzishwa na serikali ya Fuhai kwa kutumia yuan milioni 23. Kwenye kijiji hicho, kuna maji safi, umeme, barabara, simu, televisheni na mtandao wa Internet, pia kuna zahanati, maduka, shule na jumba la utamaduni, aidha, karibu na kijiji hicho, mashamba ya kilimo na ufugaji yalipangwa. Lakini wafugaji wamezoea maisha ya kuhama hama, wengi wao hawakutaki kuishi kwenye kijiji hicho. Ofisa wa kijiji hicho Bw. Jiger alisema,

"Ilikuwa vigumu kuwashawishi wafugaji kuhamia kijiji hicho kuishi maisha ya kukusanyika, kwa kuwa walizoea kuhama hama ili kufuga mifugo. Tulitangaza manufaa ya kuishi kwenye kijiji hicho kwa kila familia ya wafugaji, na kuwaambia kuwa wanaweza kuhamia kijiji hicho kwa hiari."

Bw. Adelhan na jamaa zake walijiandikisha kuhamia kijiji cha Sakru wakiwa na wasiwasi moyoni. Lakini baada ya kuhamia nyumba mpya, waliona maisha kwenye kijiji hicho ni mazuri kuliko ya zamani. Wanaweza kutumia maji na umeme bila matatizo, hata wanaweza kutumia simu na televisheni. Mbali na hayo wanapewa ruzuku na serikali. Naibu mkuu wa wilaya ya Fuhai Bw. Jialin alisema,

"Wafugaji waliohamia kijiji hicho walipata ruzuku ya yuan elfu ishirini kutoka serikali ya wilaya na yuan elfu tano kutoka serikali ya tarafa."

Familia ya Bw. Adelhan ilihamia nyumba kubwa nzuri, na ilijenga zizi la kulaza mifugo lenye eneo la mita za mraba 80, sasa hawaogopi tena maafa ya theluji. Zaidi ya hayo, walipewa shamba la hekta 10 ili kupanga nyasi na kufuga wanyama. Bw. Adelhan alishiriki kwenye semina ya kufundisha elimu ya ufugaji iliyoandaliwa na serikali ya kijiji. Alisema kwa kutumia njia ya kisayansi, anapata mapato mengi kuliko zamani. Alisema,

"Nilipata elimu nyingi kuhusu ufugaji na upandaji katika semina hiyo. Sasa ninafuga ng'ombe na mbuzi wa aina nzuri. Mapato ya familia yetu yaliongezeka kutoka yuan elfu kadhaa hadi elfu 50 kwa hivi sasa."

Mbali na ongezeko kubwa la mapato, miundo mbinu zikiwemo hospitali, shule na jumba la utamaduni kwenye kijiji cha Sakru pia imerahisisha maisha ya familia ya Bw. Adelhan. Alisema,

"Zamani hakukuwa na zahanati, nilipopatwa na ugonjwa ilikuwa lazima nitembee safari ndefu. Lakini sasa hali imebadilika, zahanati iko karibu na nyumba yangu."

Kwenye kituo cha afya cha kijiji cha Sakru, kuna daktari na mwuguzi, na dawa na vifaa vya matibabu. Miaka mitatu iliyopita, Bw. Adelhan na jamaa zake walijunga na mfumo wa ushirikiano wa matibabu vijijini, na kuweza kupata ruzuku wakitibiwa kwenye hospitali au kununua dawa.

Wafugaji wengine walipoona maisha mazuri yake, wengi wao waliamua kuhamia kijiji hicho. Mwaka jana idadi ya familia kwenye kijiji cha Sakru haikufikia 30 tu, lakini mwaka jana, idadi hiyo imefikia 60, ambapo kwenye sehemu nzima ya Altai, asilimia 30 ya wafugaji wamehamia kwenye vijiji vya kudumu."

Serikali ya sehemu ya Altai imeweka kazi ya kuwasaidia wafugaji kufanya makazi ya kudumu kuwa moja kati ya kazi tatu muhimu ya kuendeleza jamii na uchumi. Katika miaka kadhaa ijayo, serikali ya sehemu hiyo itatenga fedha zaidi katika kazi hiyo. Mkuu wa idara ya ufugaji wa serikali ya Altai Bw Ren Zhenping alisema,

"Tunachukulia kazi ya kuwasaidia wafugaji kufanya makazi ya kudumu kama njia ya kuboresha njia ya uzalishaji, kuhifadhi mazingira ya kimaumbile na kuwasaidia wafugaji kuongeza mapato, na tunatilia mkazo sana utekelezaji wa kazi hiyo."

Idhaa ya kiswahili 2008-02-27