Wafanyakazi wa Idhaa ya Kiswahili ya CRI
China Radio International
China
Dunia
(GMT+08:00) 2008-10-15 16:34:06    
Kuhusu ugonjwa wa kuhara

cri

Majira ya joto ni kipindi ambacho vijidudu mbalimbali vya tumboni vinapozaliwa, kwa hiyo majira hayo pia ni kipindi ambacho watu wengi wanapata ugonjwa wa kuhara. Katika kipindi hiki, tutawaelezeni jinsi ya kupambana na ugonjwa huo.

Bw. Li Jin ni mwalimu wa michezo katika shule ya sekondari, ana afya nzuri lakini katika mwezi mmoja uliopita alikuwa anasumbuliwa sana na ugonjwa wa kuhara.

Zamani Bw. Li Jin aliwahi kupata ugonjwa wa ghafla wa tumbo, na nusura apoteze maisha yake. Kwa hiyo safari hii baada ya kupata ugonjwa wa kuhara, mara moja alitumia mwenyewe dawa za kuangamiza vijidudu kwa siku mbili, lakini hazikusaidia hata kidogo. Bw. Li Jin alilazimishwa kwenda hospitali na kupigwa sindano kwa siku tano mfululizo, hatimaye hali yake iliboreka. Lakini baada ya siku chache tu, usumbufu wake ulirejea tena. katika siku hizo, uzito wake ulipungua kwa kilo 10 hivi.

Mkurugenzi wa idara ya magonjwa ya tumbo katika hospitali ya Xiehe ya Beijing profesa. Qian Jiaming alisema, watu wengi wana mtizamo kama Bw. Li Jin kwamba dawa za kuangamiza vijidudu zinaweza kutibu vizuri ugonjwa wa kuhara, kwa kweli mtimazo huo ni kosa. Profesa Qian alisema, ugonjwa wa kuhara una vyanzo vingi, kwa jumla vinagawanyika kwa aini mbili, yaani ugonjwa wa kuhara uliosababishwa na vijidudu na wadudu wa tumboni, aina nyingine inatokana na kupatwa na baridi, utapiamlo na magonjwa mbalimali sugu kama vile magonjwa ya ini, kongosho n.k.

Profesa Qian alisema, dawa za kuangamiza vijidudu zinaweza kutibu tu ugonjwa wa kuhara uliosababishwa na vijidudu, kwa hiyo wagonjwa wengi wa kuhara hawana haja ya kutumia dawa hizo. Profesa Qian alisema:

"si magonjwa yote ya kuhara yanatokana na kuambukizwa vijidudu, kama vile mwalimu Li, ugonjwa wake huenda unatokana na tatizo la usagaji wa chakula, dawa za kuangamiza vijidudu si kama tu hazisaidii ugonjwa wake, huenda zitaleta matatizo mapya au kutatanisha zaidi."

Profesa Qian alisema, kuna wadudu wenye manufaa kwa binadamu wanaoishi tumboni, ambao wanaweza kuzuia ukuaji wa wadudu wengine wanaosababisha magonjwa. Mwalimu Li alipotumia ovyo dawa za kuangamiza vijidudu, dawa hizo pia ziliwaua wadudu wenye manufaa na kuharibu mazingira ya ndani ya mwili, kwa hivyo ugonjwa wake ulirudia mara kwa mara.

Kwa hiyo ni ngumu kwa wagonjwa kujitafutia wenyewe sababu za kuhara bila kufanyiwa upimaji na madaktari, kutumia dawa ovyo ni hatari sana, baadhi ya magonjwa ya kuhara hata yanaweza kuambukiza. Mkurugenzi wa idara ya magonjwa ya matumbo katika hospitali ya No. 305 ya Beijing Profesa Huang Ping alisema:

"kama tatizo la kuhara likiendelea kwa zaidi ya siku 3 bila kupona hata kidogo, lazima mgonjwa aende hospitali, kwanza kuthibitisha kama ulipatwa na ugonjwa wa kuhara au la, unapaswa kufanyiwa upimaji wa kinyesi ili kutafuta vyanzo vya ugonjwa wako, halafu utaweza kupewa matibabu kutokana na chanzo cha ugonjwa wako."

Kama wagonjwa ambao hali yao si mbaya hawataki kwenda hospitali watafanyaje? Wataalamu walieleza kuwa wagonjwa kama hao wanaweza kunywa maji gram 500 yaliyochanganywa na gramu 10 za sukari na gramu 1.75 za chumvi. Kama tatizo lao likiondoka basi mgonjwa aache mara moja kunywa maji hayo. Wataalamu pia wanasema, tatizo dogo la kuhara linaweza kupona wenyewe baada ya siku 1 hadi 2, kama njia hii haisaidii basi wagonjwa lazima waende hospitali kupewa matibabu.

Aidha, sasa kumeingia majira ya Autumn, wakati huu ni rahisi sana kwa watoto kupatwa ugonjwa wa kuhara uliosababshwa na virusi vya aina ya rotavirus. Wataalamu walisema, virusi vya aina hiyo wanaweza kuishi nje ya mwili wa binadamu, kuanzia mwezi Oktoba hadi mwezi Januari ni kipindi ambacho watu wengi hupatwa na ugonjwa wa kuhara uliosababishwa na virusi hivyo.

Hivi sasa mbali na chanjo bado hakuna dawa zinazoweza kuangamiza kwa ufanisi virusi vya aina hiyo, kwa hiyo kama watoto wakiambukizwa na virusi hivyo lazima kuwapeleka hospitali kwa wakati ili kuepusha hali yao kubadilika na kuwa mbaya.

Kutokana na kuwa hakuna dawa zenye ufanisi za kuangamiza virusi hivyo, kwa hiyo kujikinga dhidi ya virusi hivyo ni muhimu sana. Mtaalamu wa kituo cha udhibiti wa magonjwa cha China Bi. Zhang Jing alisema, virusi hivyo vinaambukiza kwa njia ya kugusana, kwa hiyo hatua muhimu za kujikinga na ugonjwa huo ni kufanya vizuri kazi za usafi.